Thursday, May 30, 2013

HOTUBA YA MSEMAJI MKUU WA KAMBI YA UPINZANI MH. JOSEPH O. MBILINYI (MB)

HOTUBA YA MSEMAJI MKUU WA KAMBI YA UPINZANI MHESHIMIWA JOSEPH O. MBILINYI (MB) KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA WIZARA YA KAZI NA AJIRA KWA MWAKA 2013/2014 (Inatolewa chini ya Kanuni ya 99(9) ya kanuni za Bunge toleo la mwaka 2013)

1.0 UTANGULIZI
Mheshimiwa spika, mwaka jana nilianza hotuba yangu kwa kutoa pole kwa ndugu jamaa na marafiki  wa wale wote waliofariki dunia kwa ajali ya mv skagit, mwaka huu naomba nianze hotuba yangu kwa kutoa pole kwa ndugu jamaa na marafiki wa wale waliofariki kwa ajali nyingine ya kizembe ya kuanguka kwa ghorofa la Dar Es Salaam. Aidha, mwaka jana nilianza kwa kutoa pole kwa Mh. Joseph selasini kwa kufiwa na baba yake na mwaka huu nianze pia kwa kutoa pole kwa Mh. mchungaji Israel Natse kwa kufiwa na baba yake mzee Yohana Natse. Mwenyezi Mungu ailaze roho yake , mahali pema peponi.
Mheshimiwa Spika, hakuna ubishi wala ushindani kuwa Serikali yoyote makini duniani huweka sera na mifumo thabiti ya kuhakikisha kuwa ajira za kutosha zinatengenezwa, mazingira ya kazi yanaboreshwa na wafanyakazi wanalipwa ujira na mishahara yenye staha, si tu kwaajili ya kuwawezesha kumudu gharama za maisha, bali pia kuwapa morali wa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi kwa maendeleo ya taifa.
Mheshimiwa Spika, napenda kusisitiza kuwa  Taifa lolote duniani ambalo haliwezi kutengeneza ajira na hivyo kuwafanya vijana wake wengi wenye uwezo wa kuajiriwa kuzurura mitaani, na wale walio vyuoni wanashindwa kusoma kwa sababu ya Serikali kushindwa au kupuuza kugharamia masomo yao; sote tunatambua kuwa Taifa hili  limejaliwa rasilimali nyingi za utalii na madini ya thamani, lenye vyanzo vingi vya kodi na mapato, lakini limegubikwa na migogoro mingi, ya mara kwa mara na isiyokwisha, ya wafanyakazi wanaodai haki na mafao yao halali, huku wakiishia kunyamazishwa kwa kauli laini zenye matumaini hewa; Kwa namna yoyote ile taifa hilo, ni kielelezo cha nchi inayoongozwa na Serikali isiyo na vipaumbele, yenye viongozi wasiojali na wanaotekeleza sera wasizozijua au zilizoshindwa.
2.0 MIFUKO YA HIFADHI YA JAMII
Mheshimiwa Spika, katika Maoni yetu ya mwaka jana, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ilituhumu kwamba Serikali hii ya CCM haiijatekeleza ahadi zake kwa Watanzania kuhusu mifuko ya hifadhi ya jamii kama zilivyotajwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya 2010 – 2015. Katika Maoni hayo tulidai kwamba ahadi ya “… kurekebisha viwango vya mafao ili visipishane mno haijatekelezwa hadi sasa kwani viwango vya mafao vinavyotolewa na Mifuko mbali mbali ya Hifadhi ya Jamii ni vile vile vya kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2010.” Aidha, tulifafanua jinsi ambavyo ahadi ya “… ya kupanua wigo wa kinga ya hifadhi ya jamii ili Watanzania wengi zaidi wafaidike na huduma hiyo nayo haijatekelezwa.” Vile vile, tulionyesha jinsi ambavyo ahadi ya “kuelimisha jamii … juu ya umuhimu wa hifadhi ya jamii kwa maendeleo ya wafanyakazi na ya nchi kwa ujumla”, nayo haikutekelezwa kwa sababu Serikali yenyewe imekiri kwamba ‘“… bado kuna uelewa mdogo wa masuala ya hifadhi ya jamii kwa watunga sera, waajiri, waajiriwa, wanachama na wananchi kwa ujumla.”’
Mheshimiwa Spika, katika Maoni yetu hayo tulionyesha kwamba ahadi pekee ambayo Serikali hii ya CCM imeitekeleza ni “… kuendelea kutumia fedha za wafanyakazi zilizomo katika Mifuko mbali mbali ya Hifadhi ya Jamii kuwekeza katika miradi ambayo haina manufaa yoyote kwa wafanyakazi wenyewe.” Tulifanya rejea pana ya Taarifa Kuu ya Mwaka ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Kuhusu Hesabu za Mashirika ya Umma na Taasisi Zingine kwa Mwaka 2010/2011, iliyoonyesha kwamba “… kuna udhaifu mkubwa katika vitega uchumi vinavyosimamiwa na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii.”
Hivyo, kwa mfano, ukaguzi wa vitega uchumi vya NSSF ulionyesha kwamba licha ya Mfuko huo kuwekeza zaidi shilingi bilioni 269.272 za wafanyakazi katika ujenzi wa Awamu ya Kwanza na ya Pili ya Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), sio tu Mfuko huo ‘“… ulikuwa haujasaini mkataba na Serikali juu ya fedha za mradi huo”’, bali pia ulikuwa ‘“… haujapokea fedha ya pango, au malipo ya mkopo kutoka Serikalini ambao tayari umelimbikiza riba ya shilingi bilioni 14.157.”’

Mheshimiwa Spika, kwa kutumia Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu tulionyesha kwamba sio fedha za NSSF tu ambazo zimetumiwa na Serikali hii ya CCM kwenye UDOM. Kama tulivyosema, “… PPF imekwishazamisha jumla ya shilingi bilioni 39.987; PSPF imechakachuliwa shilingi bilioni 105.921; LAPF imepoteza shilingi bilioni 22.030; wakati ambapo NHIF imekwishaunguza shilingi bilioni 13.403 za wanachama wake. Jumla ya fedha za wafanyakazi wanachama wa Mifuko hii mitano ambazo zimeunguzwa katika ujenzi wa UDOM ni shilingi bilioni 450.615…. Vitega uchumi vyote hivi katika UDOM … havirudishi fedha za mikopo ya Mifuko husika.” Hali kadhalika, tulionyesha jinsi ambavyo ujenzi wa Jengo la Idara ya Usalama wa Taifa ulivyotafuna shilingi bilioni 11.83 za NSSF na PSPF ambazo hadi tunaandika Maoni yetu ya mwaka jana zilikuwa hazijaanza kulipwa pamoja na riba yake! Vile vile, tulionyesha kwamba jumla ya shilingi bilioni 19.77 zilitolewa kama mikopo na NSSF, PPF na LAPF kwa ajili ya ujenzi wa Ukumbi huu wa Bunge lako tukufu “… hazijalipwa hadi sasa.” Aidha, zaidi ya shilingi bilioni 152.6 zilizotolewa kama mikopo kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za Jeshi la Polisi, Machinga Complex, Continental Venture Tanzania Ltd., Meditech Industrial Co. Ltd., General Tyre, Dar es Salaam Cement Co. Ltd., Kagera Sugar, Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) na Kiwira Power Ltd. haikuwa imelipwa. Kwa sababu hizo, tulimnukuu Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali akisema “… ukubwa wa biashara inayofanywa baina ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na taasisi za Serikali na malipo yasiyokuwa na uhakika ya mikopo hiyo yanatia shaka juu ya uendelevu wa Mifuko husika katika siku chache zijazo.”
Mheshimiwa Spika, licha ya kuwa yalitokana na Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ambaye ni mteuliwa wa mhe. Rais Mheshimiwa Dokta Jakaya Mrisho Kikwete, Maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni yalishambuliwa sana na Wabunge wa CCM na wawakilishi wa Serikali yake humu bungeni. Hata hivyo, facts are very stubborn things, kama mwanamapinduzi mmoja wa karne iliyopita alivyokuwa anapenda kusema. ‘Ukweli ni vitu vikorofi sana’! Na ukweli juu ya afya ya Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii ni vitu vikorofi kweli kweli, ambavyo haviwezi kuzimwa na propaganda nyepesi nyepesi za watawala na wawezeshaji wao ndani na nje ya Bunge hili tukufu.
Mheshimiwa Spika, katika hotuba yake wakati wa Sherehe za Mei Mosi mwaka huu kule Mbeya, Rais Kikwete alielezea ‘tathmini ya afya ya kifedha’ ya Mifuko yote ya Hifadhi ya Jamii nchini kama sehemu ya ‘maboresho’ ya sekta hiyo. Tunaomba kumnukuu Rais in extenso: “Tathmini hiyo imeonesha kuwa mifuko yetu ya hifadhi ya jamii ipo kwenye hali nzuri kifedha na ni endelevu. Kwa Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSPF), Serikali itaendelea kutoa fedha kwa ajili ya malipo ya michango ya watumishi waliokuwepo kabla ya mwezi Julai 1999 mfuko ulipoanzishwa rasmi. Kwa hiyo, katika mwaka ujao wa fedha, Serikali italipa shilingi bilioni 50 ikiwa ni sehemu ya malipo hayo. Napenda kuwatoa hofu wanachama wa Mfuko huo kuwa mafao yao yako salama. Hakuna atakayestaafu akakosa kulipwa mafao yake.
“Vile vile Mamlaka ya Udhibiti na Usimamizi wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) kwa kushirikiana na Benki Kuu wameandaa na kutoa miongozo … yenye lengo la kuiwezesha mifuko ya hifadhi ya jamii kufanya uwekezaji ulio bora na wenye tija unaomnufaisha mwanachama na taifa kwa ujumla. Tangu kuanza kutumika kwa miongozo hiyo Mei 2012, uwekezaji wa mifuko hiyo umeongezeka kutoka shilingi trilioni 3.38 mpaka shilingi trilioni 4.24. Pia mali za mifuko hiyo zimeongezeka kutoka shilingi trilioni 3.74 hadi kufikia shilingi trilioni 4.73.
Mheshimiwa Spika, matrilioni haya ya Rais Kikwete yanahitaji kuchukuliwa kwa tahadhari kubwa na Bunge lako tukufu. Hii ni kwa sababu takwimu hizi zimetiliwa na shaka na Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Kuhusu Ukaguzi wa Mashirika ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2011/2012 iliyowasilishwa kwa Rais tarehe 28 Machi, 2013. Tunaomba kuiacha Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu ijisemee yenyewe: “Ukaguzi wa Mfuko wa Pensheni kwa Wafanyakazi wa Serikali Kuu (PSPF) ulibaini kwamba ‘actuarial valuation’ iliyofanyika … tarehe 30 Juni, 2010 … ilionyesha kuwa hali ya kifedha ya Mfuko iliendelea kuwa mbaya. Ukadiriaji thamani ulibaini hasara halisi ya shilingi trilioni 6.487 kwa mwaka unaoishia tarehe 30 Juni, 2010.
“Pia nilibaini kwamba katika mwaka wa fedha 2011, Serikali ilikubali kuanza kurejesha mafao yaliyolipwa na Mfuko kuanzia mwaka 2004 hadi 2010 kiasi cha shilingi za Kitanzania bilioni 716. Kiasi hiki kilipaswa kurejeshwa kidogo kidogo na Serikali kila mwaka katika mgawanyo wa shilingi bilioni 71.6 kwa muda wa miaka kumi kuanzia mwaka 2010. Kufikia mwaka unaoishia tarehe 30 Juni, 2012 kulikuwa na malimbikizo ya marejesho katika kipindi cha mwaka 2011 hadi 2012 na kufikia kiasi cha shilingi bilioni 133. Vile vile, ilibainika kwamba, Serikali ya Tanzania haikuweza kutoa fedha za kuziba pengo la upungufu uliojitokeza … ikiashiria kuwepo kwa shaka kuhusiana na uwezo wa Mfuko kuendelea kulipa madeni yake yanapokuwa tayari kwa kulipwa.
Mheshimiwa Spika, ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu kwa mwaka wa fedha uliopita inafichua ‘ukweli korofi’ zaidi kuhusu afya ya kifedha ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii hapa nchini. Hivyo basi, Ripoti hiyo inaonyesha kwamba PSPF imetoa mikopo ‘isiyolipika’ ya jumla ya shilingi bilioni 67. 179 kwa Serikali na taasisi zisizo za kiserikali “… na hakuna malipo yoyote yalifanywa kwa Mfuko katika kipindi chote cha mwaka. Hii inaweza kuharibu mtiririko wa fedha za Mfuko na matokeo yake kushindwa kulipa mafao yanapofika wakati wa kulipwa.” Taasisi zisizokuwa za kiserikali zilizofaidika na mikopo ‘isiyolipika’ ya fedha za watumishi wa Serikali hii ya CCM ni pamoja na Tan Power Resources, kampuni iliyokuwa inamilikiwa na familia ya Rais mstaafu Benjamin Mkapa na ya swahiba wake Daniel Yona ambayo iliwahi kumilikishwa Mgodi wa Makaa ya Mawe wa Kiwira kwa njia za kifisadi. Kwa mujibu wa Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu, Tan Power Resources ina ‘madeni yasiyolipika’ kwa PSPF ya jumla ya shilingi bilioni 5.421!  Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu inaeleza kwamba PSPF imeingia mkataba na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kutoa fedha za kujenga Chuo Kikuu cha Elimu Dodoma. Hata hivyo, “mapitio ya mkataba yalibaini mkanganyiko wa tafsiri ambao unahitaji kutatuliwa mapema. Kutokuwa na mkataba sahihi kunafanya kuwa na tafsiri mbali mbali ambazo matokeo yake ni hasara kwa Mfuko iwapo mgogoro utajitokeza.”
Mheshimiwa Spika, PSPF sio Mfuko wa Hifadhi ya Jamii pekee ambao afya yake ya kifedha ni ya mashaka.  Kwa mujibu wa Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu, PPF imetoa shilingi bilioni 71 katika ujenzi wa UDOM “… ingawa mkataba wa kutoa fedha kwa ajili ya mradi huu kati ya Mfuko na Serikali … bado haujakamilika hadi ripoti hii inaandaliwa.” Kwingineko katika Ripoti hiyo, inasemekana kwamba majengo ya UDOM yenye thamani shilingi bilioni 452 ‘zilizofadhiliwa’ na Mifuko ya Jamii ‘chini ya maelekezo ya Serikali’ “… hayajakabidhiwa rasmi kwa Chuo Kikuu Dodoma na Serikali ambayo ilisaini mkataba na Mifuko ya Jamii ya NSSF, PSPF, LAPF na PPF.”
Kwa kuhofia kwenda kinyume na matakwa ya kanuni ya 64(1)(d) na (e) ya Kanuni za Kudumu za Bunge, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inachelea kumwita Rais Kikwete muongo kutokana na kauli yake juu ya afya ya kifedha ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Hata hivyo, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inataka kujua, na Watanzania wanataka kujua, kati ya Rais na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ni yupi anayesema ukweli kuhusu hali ya kifedha ya Mifuko ya Hifadhi ya Afya ya Jamii katika nchi yetu? Ni nani aaminiwe na Watanzania kati ya Rais Kikwete anayesema kwamba “… mifuko yetu ya hifadhi ya jamii ipo kwenye hali nzuri kifedha na ni endelevu”; na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali anayesema kwamba “… hali ya mfuko wa hifadhi ya jamii uko katika hatari ya kutoendelea kama hatua madhubuti hazitachukuliwa na pande zinazohusika”? Aidha, wafanyakazi wa Serikali ya Tanzania wampuuze yupi kati ya Rais ‘anayewatoa hofu’ kwamba “hakuna atakayestaafu akakosa kulipwa mafao yake”; na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu anayedai kuwa kuna “… shaka kuhusiana na uwezo wa Mfuko kuendelea kulipa madeni yake yanapokuwa tayari kwa kulipwa.
Mwisho, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali hii ya CCM iwaambie Watanzania nani ni mkweli kati ya Rais Kikwete anayedai kuwa mali za Mifuko ya Hifadhi ya Jamii imefikia shilingi trilioni 4.73; na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu anayetuambia kwamba ukaguzi wake wa PSPF pekee unaonyesha ‘hasara halisi’ ya shilingi trilioni 6.487!
Mheshimiwa Spika, katika mazingira ya kiza na utatanishi kama haya, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inarudia wito wake wa mwaka jana kwa Serikali “… kusitisha mara moja matumizi haya makubwa ya fedha za wafanyakazi katika miradi ambayo inaelekea kuifilisi Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na hivyo kuhatarisha maslahi ya moja kwa moja ya wafanyakazi wa Tanzania.
Aidha, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inarudia kauli yake ya mwaka jana: “… Ni wazi kwamba Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ya Tanzania inaongozwa, kuendeshwa na kusimamiwa na watu ambao hawana uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa ujuzi na uadilifu unaohitajika kwa maslahi ya wafanyakazi wanachama wa Mifuko hiyo. Ni wazi, kwa ushahidi huu, kwamba mabadiliko makubwa ya kimfumo na kiutendaji katika Mifuko hii yanahitajika na kwa haraka kabla mifuko hii haijafilisika kabisa.”  Vile vile, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inawataka wastaafu na wafanyakazi wa Tanzania sasa waelewe chanzo halisi cha mafao yao ya uzeeni kucheleweshwa ama kutokuongezeka ama kutokulipwa kabisa na Serikali hii ya CCM! Na wakishafahamu sababu halisi za mateso yao, wastaafu na wafanyakazi wa Tanzania wachukue hatua stahiki dhidi ya wale wote ambao kwa sera zao na utekelezaji wao wa sera hizo, wamesababisha mateso hayo kwa wastaafu na wafanyakazi wetu. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaamini kwamba bila wafanyakazi kuchukua hatua hizo, maneno ya ibara ya 11(1) ya Katiba yetu kwamba “mamlaka ya nchi itaweka utaratibu unaofaa kwa ajili ya kufanikisha utekelezaji wa haki ya mtu … kupata msaada kutoka kwa jamii wakati wa uzee, maradhi au hali ya ulemavu, na katika hali nyinginezo za mtu kuwa hajiwezi …” yatabaki dhihaka ya kikatili kwa wastaafu na wafanyakazi wetu.
Mheshimiwa Spika, aidha Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kurejea pendekezo letu tuliloishauri katika bajeti ya Wizara hii ya mwaka 2011/2012 katika kuona umuhimu wa kuiunganisha mifuko yote ya hifadhi za jamii na kubaki katika wizara moja ambayo ni ya Kazi na Ajira. Kambi rasmi ya Upinzani inasisitiza kuwa lengo kuu la kuunganisha mifuko hii ya hifadhi za jamii ni katika kuirahisishia Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Hifadhi za Jamii (SSRA) katika kutekeleza Sheria moja na kuunda vifungu sawa vya kisheria vitakavyosimamia utekelezaji na uendeshaji wa mifuko hii ambapo kwa sasa mifuko hii imekuwa chini ya wizara tofauti na hivyo hata utekelezaji wake unakua mgumu na kuleta ukinzani kwa Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Hifadhi za Jamii. Tunasisitiza kuwa pendekezo letu ni kuifanya PPF na NSSF iunganishwe na kuwa mfuko mmoja kwaajili ya Sekta Binafsi vilevile LAPF, PSPF na GEPF iunganishwe na kuwa mfuko mmoja kwaajili ya Sekta ya Umma. Pia, kambi ya Upinzani inapendekeza mifuko yote isimamiwe chini ya Wizara ya Kazi na Ajira.
3.0 NYONGEZA YA MISHAHARA YA WAFANYAKAZI NCHINI
Mheshimiwa Spika, Katika hotuba yake ya Mei Mosi mwaka huu, Raisi Kikwete alisema kuwa " ........Kwa upande wa makusanyo ya kodi kwa mfano,mapato yameongezeka kutoka wastani wa shilingi bilioni 541 kwa mwezi mwaka 2011/12 hadi kufikia shilingi bilioni               637 kwa mwezi mwaka 2012/13, ikiwa ni ongezeko la asilimia 18.  Mapato yanapoimarika kama hivi, Serikali          inakuwa na uwezo mkubwa wa kuwahudumia wananchi wake, kutekeleza miradi ya maendeleo  na wakati huo huo             kuboresha zaidi maslahi ya wafanyakazi........  Pamoja na             mafanikio hayo, lakini bado hatujafikia mahali ambapo tunaweza kuongeza mishahara kama vile ambavyo             tungependa sote tupate.  Hata kwa kiwango cha sasa ambacho sote tunakubaliana hakitoshi bado mishahara             inachukua sehemu kubwa ya mapato ya Serikali."
Mheshimiwa Spika, kitendo cha Raisi kusema kuwa mishahara itaongezwa bila ya kutaja kiwango kama ilivyo desturi ya mei mosi haitoshi. Ni lazima Serikali iseme kiwango cha nyongeza ya  mshahara kwa wafanyakazi nchini kwa mwaka ujao wa fedha wa 2013/2014 ni kiasi gani, na je nyongeza hiyo itatatua matatizo ya wafanyakazi kwa kiwango gani? Aidha, kambi rasmi ya Upinzani Bungeni, inaiona kauli ya Mheshimiwa Raisi kuwa, Serikali imedhibiti ubadhirifu wa umma, ni lazima ionekane katika mishahara ya wafanyakazi wa sekta zote za umma na za binafsi.
4.0 PUNGUZO LA KODI YA MAPATO KWA WAFANYAKAZI PAYE)
Mheshimiwa Spika,Pamoja na ugumu wa mazingira ya kazi, mishahara duni na hali ngumu ya maisha nchini, bado mfanyakazi anaendelea kunyonywa kwa kiwango kikubwa cha PAYE , ambacho ni moja ya vyanzo vya Serikali katika mapato, huku Serikali ikishindwa kutafuta njia nyingine mbadala za kukusanya kodi ikiwemo  kufuta misamaha ya kodi isiyo na tija kwenye uchumi wa taifa letu.
Mheshimiwa Spika, katika maoni yetu ya mwaka jana, tulipendekeza kwamba kiwango cha PAYE ishuke kutoka asilimia 14 za sasa hadi asilimia 9 kwa kiwango cha chini kinachotozwa na asilimia 27 kwa kiwango cha juu kinachotozwa.Katika hotuba yake ya mei mosi, zaidi ya kusema kwamba serikali imekamilisha uchambuzi wa maombi ya wafanyakazi na kwamba waziri wa fedha atayafafanua zaidi katika hotuba yake ya bajeti, Raisi Kikwete hakusema kodi ya pato la mfanyakazi itapungua kwa kiasi gani. Kwa kuzingatia mapendekezo ya TUCTA kwamba kima cha chini cha mfanyakazi wa Tanzania kiwe 350,000, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inapendekeza kwamba kiwango cha chini cha mshahara kitakachotozwa PAYE kiwe shilingi 350,000. Hii itawezesha wafanyakazi wote wanaopata kiwango hicho cha mshahara au pungufu yake kuwa na mapato zaidi na kukabiliana na mfumuko wa bei wa mara kwa mara na kupanda kwa gharama za maisha.
Mheshimiwa Spika,wakati Serikali hii ya CCM ikisita kupunguza mzigo wa maisha magumu unaowakabili wafanyakazi, kwa kuwaongezea mshahara au kuwapunguzia PAYE , Serikali hiyohiyo haijawahi kusita kutoa misamaha ya kodi kwa waajiri matajiri wa wafanyakazi. Ukweli ni kwamba katika baadhi ya sekta  zinazoongoza kwa mauzo ya fedha za nje waajiri wamelipa kodi ya mapato ya chini kuliko kodi ya PAYE wanayolipa wafanyakazi wao licha ya waajiri hao kuwa na vipato vikubwa kutokana na mauzo ya bidhaa zao nje ya nchi. Kwa mfano, kwa mujibu wa hotuba ya bajeti waziri wa nishati na madini iliyowasilishwa na  waziri mwenye dhdamana, Mh. Prof.  Muhongo, katika kipindi cha miaka 14 (1992-2012), makampuni ya madini yalilipa jumla ya shilingi bilioni 468 kama kodi ya mapato. Katika kipindi hicho hicho, wafanyakazi wao walilipa jumla ya shilingi bilioni 506  kama PAYE na tozo ya kuendeleza ujuzi (Skills Development Levy) inayolipwa VETA. Takwimu hizo zinaonesha kwamba, katika miaka sita ya kwanza (1999-2004) makampuni ya madini yalilipa shilingi 0 kama kodi ya mapato, wakati waajiriwa wao wa kitanzania walilipa shilingi bilioni 52 kama PAYE na SDL (Skills Development Levy).Aidha,katika miaka 8 iliyofuata ,makampuni ya madini yalilipa kodi ya mapato ya shilingi bilioni 468 wakati waajiriwa wao walilipa shilingi bilioni 454. Kwa kipindi chote hicho kwa mujibu wa takwimu hizo  za Mh. Prof Muhongo,thamani ya madini yaliyouzwa nje ya Tanzania na makampuni hayo ilikua ni shilingi Trilioni 19.278. Kwa takwimu hizi, sio tu kwamba Serikali hii ya CCM imeruhusu utajiri wa nchi hii kutajirisha makampuni ya kigeni bali pia imewanyonya waajiriwa wa kitanzania wa makampuni hayo kwa kuwatoza kodi kubwa ya mapato kuliko inayolipwa na waajiri  wao wa kigeni.
4.1 Serikali na kima cha chini cha mishahara sekta binafsi Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2012/2013 katika kifungu 2001 wizara ilitenga jumla ya shilingi 60,000,000 kwa ajili ya kuratibu na kuwezesha utafiti wa kima cha chini cha mshahara katika sekta binafsi , na pia zilitengwa shilingi 55,000,000 kwa ajili ya vikao vya bodi 12 za kisekta za kima cha chini cha mshahara katika seka binafsi na mwaka huu wa fedha 2013/2014  katika fungu hilo hilo zimetengwa kiasi cha shilingi 60,600,000 kwa ajili ya ‘kuratibu na kuwezesha utafiti wa kima cha chini cha mshahara katika sekta binafsi’, vile vile zimetengwa tena shilingi 22,325,000 kwa ajili ya ‘kuwezesha vikao vya Bodi 12 za kisekta za kima cha chini cha mshahara katika sekta binafsi’. Yaani kwa miaka 2 tumetumia jumla ya shilingi 197,925,000 kwa ajili ya kufanya kinachoitwa utafiti na vikao kwa ajili ya kujua kama sekta binafsi inahitaji kuongezewa mishahara ama laa na kama ipo haja iwe ni kiasi gani .
Kambi rasmi ya upinzani , inasikitishwa sana na mtindo wa serikali hii sikivu ya CCM ambayo inasema kuwa inasikia lakini inaendelea kutenga fedha za kufanya utafiti kuhusiana na kima cha chini cha mishahara ya wafanya kazi, hivi ni kweli kuwa serikali hii haijui wafanyakazi wanastahili kulipwa nini , hivi ni kweli kuwa hamkuwasikia TUCTA tangu mwaka 2010 walipopendekeza kuwa kima cha chini cha mshahara kiwe kiasi gani? Hivi hamjui kuwa gharama za maisha zimepanda sana na hivyo huhitaji kufanya utafiti kujua kama wafanyakazi wa sekta binafsi wanahitaji kuongezewa mishahara?
Aidha kwa maombi mapya ya kutengwa kwa kiasi hiki cha fedha kinatoa taswira kuwa, hata kauli aliyoitoa Mhe. Raisi kwenye maadhimisho ya Mei Mosi mwaka huu kwa kusema nanukuu " Katika kikao chetu tulichokutana na viongozi wa TUCTA tarehe 27 Februari, 2013 tulijadili suala hili na kukubaliana kwamba Serikali iendelee kulichambua zaidi ili kutoa unafuu zaidi kwa wafanyakazi kila mwanya unapopatikana.  Nafurahi kuwaarifu kuwa kazi ya uchambuzi imekamilika na maombi yenu yamesikilizwa." Hii ni fedheha kwa Serikali  makini na sikivu ya CCM, ambayo utendaji wake na kauli za viongozi wake wakuu ni wazi zinalenga kuwalaghai wafanyakazi na kuwanyonya kupitia matumizi mabaya ya kodi zao!
5.0 TATIZO LA UKOSEFU WA AJIRA NCHINI
Mheshimiwa Spika, Tatizo la ukosefu wa ajira limeendelea kukua kila kukicha huku likiambatana na ugumu wa maisha. Upatikanaji wa ajira katika soko la ajira nchini ni wa kusikitisha na jambo la kushangaza ni kuwa Serikali haitaki kukubali kuwa tatizo hili ni kubwa sana na lina athari kubwa si kwenye jamii ya kitanzania bali hata kwenye uchumi wa taifa hili.
Leo hii tukiwa tumefungua milango ya ushirikiano baina ya nchi wanachama wa Jumuia ya Afrika Mashariki, kama taifa hatujaweka mikakati ya jumla ya kukabiliana na changamoto za soko la ajira katika Jumuia. Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni, inajiuliza kuwa wakati leo mfumo wa elimu wa Tanzania ukiwa katika hali tete yenye kuzalisha kizazi kisichoweza kushindana na nchi za Kenya, Rwanda, Uganda ambapo wazazi wengi wenye uwezo wanapeleka watoto wao huko, je nchi ipo tayari kukabiliana na vigezo takwa vya soko la ajira la ujumla? Ndio maana leo hii si ajabu kukuta katika soko la ajira, hasa katika utalii kwenye mikoa ya kaskazini kama Kilimanjaro na Arusha, wakenya wameweza kuliteka soko la ajira ya utalii kama waongoza watalii, wafanyakazi wa mahoteli makubwa ya kitalii huku watanzania wakishindwa kutumia fursa hizo kutokana na changamoto za kitaaluma ambazo zimesababishwa na mfumo duni wa elimu nchini.
Mheshimiwa Spika, Ili nchi iweze kufanya mabadiliko makubwa katika sekta ya ajira, lazima Serikali ikubali kuwa mfumo wa elimu uliopo sasa haukidhi matakwa ya soko la ajira duniani. Mfumo wa elimu uliopo hauzalishi wataalamu wa kutosha wa fani mbalimbali wanaoweza kufanya kazi kwa weledi katika sekta mbalimbali ndio maana hata kwenye sekta ya madini nchini, leo hii asilimia kubwa ya kazi zenye kuhitaji ujuzi na sifa za juu, zimeendelea kufanywa na wageni na bila kufuata sheria za nchi.
Mheshimiwa Spika, Ili tufanikiwe katika soko la ajira hatuna budi kufumua mfumo mzima wa elimu yetu. Hakuna mabadiliko magumu duniani, kama madadiliko ya mfumo wa elimu kwa kuwa unahusisha gharama kubwa, wakati na hata kuleta mtikisiko kwa kuwa utaathiri hata ajira za wale waliopo; lakini pia wataalamu wanakiri kuwa mabadiliko ya mfumo wa elimu ndio njia pekee ya kuweza kukabiliana na changamoto kubwa za kiuchumi, kijamii, kisiasa na hata kiutamaduni. Lazima kama taifa , tukubali kufanya maamuzi magumu ili kuokoa nchi yetu ambayo sasa imekosa mikakati endelevu ya kukabiliana na tatizo la ajira. Kambi rasmi ya Upinzani inajua kuwa jibu la Serikali katika kupambana na tatizo la ukosefu wa ajira litakua "mtikisiko wa uchumi duniani umeathiri nchi nyingi hata zilizoendelea nazo lina tatizo la ukosefu wa ajira".
Mheshimiwa Spika, tumekuwa tukishuhudia serikali ikiwatimua wafanya biashara wadogo walioamua kujiajiri wenyewe na hivyo kuwakosesha amani na kuwakatisha tamaa.Cha kusikitisha zaidi ni kwamba; Serikali imekuwa ya kwanza kuzikimbia bidhaa zinazozalishwa na watanzania hawa wanaojitahidi kutatua tatizo (la ukosefu wa ajira kwa kujiajiri wenyewe), na kukimbilia bidhaa za nje licha ya kuwa bidhaa zinazozalishwa na watanzania zipo za kutosha na zenye hadhi na ubora wa kutosha.Hivi serikali haioni tunawakatisha tamaa hawa watanzania ambao wameamua kujiajiri?
6.0 UKOSEFU WA AJIRA KWA VIJANA NCHINI
Mheshimiwa Spika, Tanzania, tumebarikiwa kwa kuwa na rasilimali nyingi, lakini asilimia kubwa ya watanzania imeendelea kuishi katika umasikini mkubwa , huku soko la ajira kila mwaka likikua katika upande wa sekta ya kilimo na sekta isiyo rasmi ambapo kuna kiwango kidogo cha ujira na uzalishaji.
Mheshimiwa Spika,tatizo la ajira nchini limeendelea kukua, huku viongozi wa Serikali wakiendelea kupoza wananchi kuwa tatizo la ajira si kubwa na kuwa Serikali imefanya jitihada katia kuongeza ajira nchini. Leo hii, tunashuhudia ongezeko la ajira , lakini ajira zisizo na tija kwa taifa, ajira zisizo za staha kwa watanzania na ajira zisizo na ujira wa kuridhisha kwa watanzania, Je tuendelee kujisifia kuwa tunajenga jamii yenye usawa na kuheshimu utu na thamani ya mtanzania?
Mheshimiwa Spika, Serikali ya CCM iliahidi mambo mengi kwa mbwembwe ili kupata kura mwaka 2010, wakati ahadi zake kwa wananchi walizotoa kwa mwaka 2005 zikiwa zimetekelezwa kwa kiwango kidogo. Mojawapo ya ahadi hizo ni pamoja na ajira milioni moja za Raisi Kikwete alizowaahidi wapiga kura. Serikali inayoongozwa na CCM haina budi kutambua kuwa ari na mwamko wa watanzania leo hii si kama wa wakati ule wa "Ndiyo mzee", kwa kuwa watanzania sasa wamenguka na wanaelewa wajibu wao katika kuisimamia Serikali.
Mheshimiwa Spika, tatizo la ajira nchini ni kubwa sana na Serikali isipokubali wazi kuwa hali ni mbaya na kuamua kuweka mkakati wa kitaifa wa kukabiliana na tatizo hili, ni wazi kuwa, tunajichimbia kaburi , kwa kuwa uchumi wetu utaendelea kuporomoka huku asilimia kubwa ya watanzania wakiishi katika maisha magumu yanayoambatana na maumivu ya kupanda kwa gharama za maisha. Leo hii, tunasema zamani mtu akiokota chupa na makopo ya plastiki barabarani ama kwenye majalala, ni mwendawazimu, ila tulipofikia hata wazazi wetu, wazee ambao hawana pensheni na wanaishi kwa mazingira magumu, wameingia mitaani na kuanza kuokota makopo kama sehemu ya ajira kwao. Wazee wetu wanaokota makopo, vijana wanaokota makopo, watoto wanaokota makopo, kwa kuwa taifa sasa limekosa mwelekeo wa kuweza kuandaa mazingira kwa wazee, vijana na watoto katika kujikwamua kimaisha kwa mipango endelevu ya kazi na ajira nchini.
Mheshimiwa Spika, kati ya mambo ambayo yamesababisha ukosefu wa ajira nchini ni pamoja na kutolingana kwa uhitaji na  upatikanaji wa wa ajira katika soko lo ajira, uanzilishwaji wa ajira katika shughuli za uchumi unaotokana na sera  zisizotekelezeka za uwekezaji, kutokuwepo kwa programu mbalimbali za ajira zinazoweza kuchangia upatikanaji wa ajira katika sekta mbalimbali kuanzia ngazi ya taifa mpaka serikali za mitaa.
Mheshimiwa Spika, Moja ya changamoto kubwa ambayo vijana wengi wa kitanzania tunakutana nazo ni pamoja na kukosa elimu, maarifa, mafunzo na ujuzi unaotakikana katika soko la ajira hapa nchini na katika jumuia ya Afrika mashariki. Wakati huohuo, kazi nyingi zinatoa na ajira zisizoleta tija zenye masharti magumu. Kiuhasilia, kuna matatizo mengi ya kimuundo na vikwazo vinavyofanya ajira kwa vijana na uwezekano wa vijana kuajiriwa kuwa mgumu. Waajiri wengi, kwa mfano wanatoa matangazo ya nafasi za kazi na ajira kwa kuweka vigezo kama ujuzi wa kazi wa kuanzia miaka mitano na kuendelea, wakati vijana wengi, kama inavyjulikana, hawana uzoefu wala ujuzi katika ajira hizo zinazotangazwa ingawa wana uwezo wa kuzifanya na kuzitekeleza. Ingawa , waajiri wote katika sekta binafsi na umma, wanaweka masharti au vigezo vya ujuzi na uzoefu kuwa moja ya masharti magumu ya ajira kwa vijana, wanasahau kuwa  Tanzania tumekosa mpango maalumu wa mafunzo yanayoendana sambamba na elimu ya kijana, ili kumfanya kijana apate ujuzi katika taaluma yake na katika sekta inayohusika. Hali hii inasababisha ugumu kwa waajiri, katika kutoa nafasi za kwa kazi kwa vijana, kwa kuwa kuajiri mtu asiye na ujuzi au uzoefu inachukuliwa kama ni gharama, kwa kuwa mwajiri lazima aingie gharama za kutoa mafunzo ya awali tena kwa vijana atakaoajiri. Hii inasababisha waajiri wengi kukwepa kuwaajiri vijana kwa kigezo cha kupunguza gharama za mafunzo.
Mheshimiwa Spika, tatizo la ajira kwa vijana pia linachangiwa  zaidi kwa kutokuwa na uoanishaji  mzuri na ushirikiano kati ya taasisi za elimu na mafunzo kwa upande mmoja na viwanda au soko la ajira kwa upande mwengine. Na hii ni kwa kuwa, mitaala ya sasa ya elimu na mafunzo haindeshwi kwa kushirikisha wadau wengine, hasa katika masuala ya kazi na ajira. Mabadiliko makubwa ya kisera yanatakiwa kufanyika katika sekta mbalimbali ambazo zina msukumo katika kuongeza thamani ya ya mtafuta kazi kwenye soko la ajira . Kati ya maeneo ya muhimu ambayo yanatakiwa kufanyiwa mabadiliko ni pamoja na kuazimia kufanya mabadiliko katika mfumo wa elimu uliopo sasa kwa  kufanya maboresho kwanza; kwa kuhakikisha kuwa elimu ya msingi na sekondari inatolewa bure  kwa watanzania wote. Pili mfumo na mtaala wa elimu uliopo sasa urekebishwe ili uweze kukidhi mahitaji ya soko la ajira ambalo huwa linabadilika. Lazima Serikali kwa kupitia wizara ya elimu na mafunzo ikubali kufanya mapinduzi ya sera ya elimu itakayomfanya kijana wa kitanzania aweze kuajiriwa popote pale hasa katika jumuia ya Afrika Mashariki. Lakini pia ni kwa Serikali kuhakikisha mipango na mikakati ya ukuzaji wa  sekta mbalimbali inaambatana  na uanzishwaji wa kazi na ajira kwa vijana wa kitanzania. Kila sekta iendane na mipango endelevu ya kukuza ajira kwa vijana. Kwa mfano ukuzaji wa sekta ya miundombinu, uendane na kutoa nafasi za ajira kwa vijana wa kitanzania pamoja na kuwalipa mishahara na posho zenye staha, zitakazowezesha vijana kujikwamua na hali ngumu ya kiuchumi na maisha.
Mheshimiwa Spika, ushindani wa kidunia, unafanya uchumi wa nchi mbalimbali kuendana na mabadiliko mbalimbali, hasa mabadiliko ya teknolojia. Hapa nchini, tumeshuhudia mabadiliko makubwa na mapinduzi ya teknolojia kuanzia kwenye uzalishaji, kilimo, habari na mawasiliano. Mabadiliko makubwa yanayoendelea katika vigezo na masharti ya kazi, ni kiashiria kikubwa kuwa vijana lazima wasaidiwe katika kukabiliana na changamoto za ukuaji wa  kasi wa teknolojia. Hata vijana ambao wanapata fursa ya ujasiriamali lazima wapate mafunzo ya kukabiliana na ukuaji wa teknolojia.
Mheshimiwa Spika, kutokana na ahadi mbalimbali ambazo zilitolewa kipindi cha uchaguzi  wa mwaka 2010 za kuongeza ajira kwa vijana na kukabiliana na tatizo la ukosefu kwa ajira za vijana, ikiwemo kutatua changamoto za vijana waliopo katika sekta isiyo rasmi ;wamachinga, wachuuzi wa bidhaa ndogondogo,wakulima wadogowadogo,wasanii,wavuvi,wajasiriamali,mamalishe, wafanyabiashara ndogondogo, wachimba madini, waliopo kwenye sekta ya utalii; matumaini ya vijana wengi yalikua ni utekelezaji wa ahadi za Serikali kwa wakati. Pamoja na taifa kuwa na takribani ya vijana milioni 16, ambapo katika kupitisha bajeti ya vijana, fedha zilizotengwa kwa ajili ya vijana zilikua ni kiasi kidogo cha bilioni 3.
Mheshimiwa Spika, Katika kuweka fursa sawa kwa wote na kuleta usawa katika mgawanyo wa rasilimali za nchi hii, kwa tengo hilo la fedha za kiasi cha bilioni 3 kwa vijana milioni 16 wa kitanzania, basi kila kijana ana uwezekano wa kupata kiasi cha shilingi za kitanzania 187.5 kama mtaji.
Mheshimiwa Spika,  Huu si upotoshaji kama mnavyouita bali ni ukweli halisi ambao watanzania leo wanakumbana nao kwa kuwa na Serikali ambayo haina vipaumbele katika kukabiliana na tatizo la ajira kwa vijana. Kumekua na ongezeko la vijana wanaojihusisha na biashara za madawa ya kulevya, ujambazi, ukahaba, hali inayochangiwa na fursa chache za kufikiwa kwa malengo na miradi mbalimbali ya programu za vijana.
Mheshimiwa Spika, jitihada za kutengeneza mazingira kwa vijana na watanzania kwa ujumla hasa wanaofanya biashara katika maeneo yasiyo rasmi maarufu kama wamachinga, unaleta changamoto katika uchumi wa taifa letu na katika utatuzi wa migogoro inayotokana na ukosefu wa ajira nchini. Serikali inatakiwa kuweka mpango mkakati wa kuoanisha idadi ya vijana ambao wamekuwa wakifanya biashara zao katika maeneo yasiyokubalika,na  kuwatengea maeneo ambayo yatawakutanisha na wateja wao ili waendeshe biashara zao bila bughuza kwa wengine. Hii iambatane na mifumo dhabiti ya kuhakikisha kuwa vijana wanapata fursa ya mikopo katika taasisi za fedha nchini yenye masharti nafuu.
Mheshimiwa Spika, kuna haja ya Serikali kuanzisha mpango wa kuwadhamini vijana waliotimiza masharti ya kibiashara inayoambatana na michanganuo kwa kushirikiana na Benki ambazo zina matawi mpaka sehemu za vijijini, ili mipango ya kifedha ya kuwanufaisha vijana iwafikie kwa ukaribu na kwa wakati ili kukabiliana na tatizo la ajira kwa vijana hapa nchini.
Mheshimiwa Spika, tatizo la ajira nchini bado ni kubwa sana na linazidi kuwa siku hadi siku huku kukiwa hakuna ufumbuzi wa kuaminika unaotolewa na viongozi wa nchi.Vijana wamekuwa wakiendelea kuhitimu katika vyuo mbali mbali nchini huku wakiwa wanakosa kazi maalum za kufanya na hivyo kujikuta wakiishi maisha ya dhiki na yasiyotamanika huku wakiwa wamekata tamaa. Katika jitihada za kutatua tatizo la ukosefu wa ajira nchini,wataalam mbalimbali wamekuwa wakishauri kwamba suluhisho la kuwanusuru vijana ni kuwahamasisha na kuwajengea mazingira ya kujiajiri wenyewe kwenye sekta binafsi kama ufundi,kilimo, ujasiriamali na kadhalika.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ni dhahiri kuwa vijana wengi wameendelea kuhitimu elimu ya juu nchini kila mwaka katika fani mbalimbali. Pamoja na ugumu wa soko la ajira nchini,lazima Serikali iweke mikakati ya kuhakikisha kuwa kundi hili linapewa elimu na mafunzo ya kuwawezesha kutumia taaluma zao ili waweze kusaidia kada mbalimbali nchini.Moja ya mikakati ambayo Serikali inaweza kuitumia ni pamoja na kuingia ubia na makampuni yaliyo katika sekta mbalimbali nchini ambazo zitakua zinatoa nafasi za mafunzo ya kazi 'internship' kwa muda utakaopangwa kama moja ya wajibu wa mashirika kwa umma 'Corporate Social Responsibility'. Hii si tu itawajengea vijana uwezo wa kujifunza bila pia italisaidia taifa kutunza thamani ya mtaji rasilimali watu(Human Capital Value) na kuwa taifa lenye ujuzi na maendeleo ya nguvu kazi (human resoures development ).Lazima serikali sasa itambue kuwa kundi vijana ndilo chachu ya mabadiliko ya kila kitu hivyo wakishirikishwa ipasavyo katika sekta mbalimbali wanao uwezo wa kuliletea maendeleo ya kweli taifa hili.Kama serikali haitakuwa makini katika kuutafutia ufumbuzi mgogoro huu wa ajira, ni wazi kuwa  vijana wataendelea kudai mabadiliko hata kwa kutumia nguvu pale inapobidi kutokana na ugumu wa maisha na ufinyu wa fursa za kuwakwamua kimaisha.
6.1 UKOSEFU WA AJIRA KWA MAKUNDI MAALUMU NA CHANGAMOTO ZAKE ZA KISERA.
Mheshimiwa Spika, Kambi rasmi ya upinzani inaendelea kuitaka Serikali kuboresha sera za kazi na ajira, sera za usalama wa mahali pa kazi pamoja na sheria mbalimbali ambazo zitatoa nafasi na fursa kwa makundi maalumu yalipo katika jamii yetu. Ukiangalia mifumo mbalimbali ambayo ipo nchini, kuanzia mifumo ya elimu, mifumo ya kifedha na mifumo ya uendelezaji wa mtaji watu, makundi maalumu hasa walemavu wamekua wakikumbana na changamoto nyingi ambazo zimewakatisha tamaa. Soko la ajira na kazi leo, halijawekea mfumo utakaohakikisha kuwa unatoa fursa kwa walemavu ili nao wapate nafasi zaajira na majukumu ya kazi yatakayoweza kuwaendeleza na kujikwamua kiuchumi.
Mheshimiwa Spika,katika mawasilisho ya bajeti kwa wizara hii kwa mwaka wa fedha wa 2012/2013 , waziri alieleza kuwa kwa  jumla ya watu wenye ulemavu 308[1] walipatiwa mafunzo ya  ujuzi wa fani mbalimbali kwa kupitia mafunzo ya ujuzi kwa kushirikiana na wadau kama CCBRT(Comprehensive Community Based Rehabilitation in Tanzania), CEFA na Radar Development ambapo kati ya wahitimu hao 145 wameajiriwa na 163 wamejiajiri.
Mheshimiwa Spika, idadi hii haileti taswira halisi ya makundi maalumu katika jamii ambayo yana watanzania wenye elimu, ujuzi na utaalamu katika fani mbalimbali lakini wamekosa fursa za ajira kutokana na hali zao. Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka wizara kutoa takwimu ya jumla ya watanzania walio kwenye makundi maalumu walioajiriwa katika sekta mbalimbali na waliojiajiri pamoja na kutoa tathmini ya ufuatiliaji wa utekelezwaji wa Sera ya Taifa ya Ajira ya mwaka 2008 katika kuhakikisha kuna usawa wa fursa za ajira na kipato kwa makundi yote. Kambi rasmi ya upinzani inataka kujua ni kiasi gani cha fedha za maendeleo amacho wizara imetenga kwa mwaka huu katika kuwawezesha walemavu nchini katika kukabiliana na changamoto za maisha aidha kwa kuwaanda kujiajiri ama kwa kuwaongezea ujuzi na maarifa ili waweze kuajiriwa.
6.2 TATIZO LA AJIRA MBAYA KWA WATOTO NA ATHARI ZAKE
Mheshimiwa Spika, kwa miaka mingi haki za watoto zinakiukwa hasa katika suala la kuwaajiri kinyume cha umri wao, ambapo kimsingi ni kosa na ni kinyume na sheria na taratibu za nchi.Hali hii inachangiwa na ugumu wa maisha hasa kwa watoto wanaoishi vijijini na wale ambao wamekumbana na athari mbalimbali ikiwemo wale ambao wazazi wao wamefariki kutokana na ugonjwa wa UKIMWI. Zaidi pia inatokana na hali mbaya ya umasikini uliokithiri katika familia nyingi za kitanzania, hali inayomnyima mtoto kufanya maamuzi sahihi kutokana na umri wake na hivyo kukimbilia kwenye ajira hatarishi kwa misingi ya kujikomboa kiuchumi.
Mheshimiwa  Spika, lakini ni wazi kuwa watoto walio katika ajira mbaya wananyimwa elimu na fursa ya kukua na kujenga vipaji na uwezo utakaoweza kuwakwamua wao, familia na jamii zao kutoka kwenye mzunguko wa umaskini. Tumeshuhudia ajira mbaya za watoto ambao wengi wanafanya ajira hatarishi na zenye kuleta madhara si tu ya kiafya bali kisaikolojia ikiwemo ajira za kwenye mashamba makubwa ya kahawa, chai, tumbaku; ajira za viwandani; ajira za kazi za nyumbani; ajira hatarishi kwenye migodi ya madini na machimbo na kadhalika. Hii si tu ni hatari kwa taifa ambalo tunasema watoto ni taifa la kesho, bali kwa mustakabali wataifa ambalo lina amini katika misingi ya haki na usawa pamoja na kuwalinda watoto dhidi ya mazingira hatarishi.
Mheshimiwa Spika,katika kukabiliana na tatizo la ajira mbaya kwa watoto,mwezi Machi mwaka huu , Marekani ilitoa ruzuku ya Sh. bilioni 16 kwa Kamati ya Uokoaji wa Kimataifa nchini (IRC) kwa ajili ya kukabiliana na ajira mbaya kwa watoto katika mikoa ya Kigoma na Tanga ambapo fedha hizo zitatumikakupitia kwenye mradi mpya ujulikanao kama ”Wekeza” na kuwa IRC itashirikiana na wabia wake kukabiliana na ajira kandamizi na za kinyonyaji dhidi ya watoto.
Mheshimiwa Spika, Balozi Lenhardt alikaririwa akisema  kuwa “Mradi utalenga wilaya sita katika mikoa ya Kigoma na      Tanga ambako kuna tatizo kubwa la utumikishwaji wa                      watoto katika ajira mbaya kwenye shughuli za kilimo na kazi       za majumbani na utawahudumia waathirika pamoja na        kujenga uwezo wa serikali kulishughulikia tatizo hilo,”
Mheshimiwa Spika, pamoja na msaada wa Marekani katika kukabiliana na ajira mbaya kwa watoto, Serikali kwa kupitia wizara itupatie majibu ni mkakati gani uliowekwa katika kukabiliana na ajira mbaya kwa watoto katika sehemu mbalimbali za taifa hili tofauti na wilaya hizo 6 zilizofadhiliwa na Marekani.
7.0 PENSHENI KWA WAZEE WOTE NCHINI
Mheshimiwa Spika;  katika maoni yake kuhusu bajeti ya Serikali na Ofisi ya Waziri na Wizara ya Kazi na Ajira ya mwaka 2011 na 2012 kwa nyakati mbalimbali Kambi Rasmi ya Upinzani inayoongozwa na CHADEMA imeitaka Serikali kuharakisha kuanza kutoa pensheni kwa wazee wote nchini.
Mheshimiwa Spika; majibu ya Serikali hii inayoongozwa na CCM yamekuwa ni ahadi kwa wazee kwamba pensheni hiyo itaanza kulipwa kwa kuwa serikali iko katika hatua ya mwisho ya kufanya utafiti na kuandaa mfumo wa kisheria.
Mheshimiwa Spika; tarehe 6 Agosti 2012 wakati akijibu maswali bungeni hatimaye Waziri wa Kazi na Ajira Gaudencia Kabaka akatoa ahadi mahususi kwamba mwanzoni mwa mwaka 2013 ingetungwa sheria ya wazee ambayo pamoja na mambo mengine ingeweka mfumo madhubuti wa wazee wote kuanza kulipwa pensheni kuanzia mwaka huu wa 2013. Waziri alilihakikishia Bunge kwamba Serikali iko katika hatua za mwisho za kuandaa mpango madhubuti wa ulipaji wa pensheni kwa wazee nchini kuanzia mwaka 2013.
Mheshimiwa Spika; badala ya kutimiza ahadi hiyo huku mwanzoni mwa mwaka 2013 ukiwa umepita bila sheria husika kutungwa wala pensheni kuanza kulipwa, Rais Jakaya Kikwete akihutubia kilele cha wiki ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii Mkoani Dodoma tarehe 17 Mei 2013 aliagiza Wizara ya Kazi na Ajira kuanza ‘kufikiria’ kuwalipa pensheni wazee wote na kujiridhisha kabla ya kuanza kutoa mafao hayo.
Mheshimiwa Spika; kufuatia agizo hilo la Rais, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inayoongozwa na CHADEMA inaitaka Wizara ya Kazi na Ajira itoe taarifa ya kina kwa Bunge kueleza Mpango Madhubuti ambao ilijibu bungeni kwamba uko katika hatua za mwisho umeishia wapi na kuwasilisha bungeni rasimu ya mpango huo iliyokuwa tayari mpaka wakati Waziri alipojibu bungeni mwaka 2012. Aidha, Wizara ya Kazi na Ajira ieleze juu ya matumizi ya fedha za umma zilizotumika kufanya tathmini na utafiti ambao Wizara ilieleza katika majibu yake ya wakati uliopita iwapo ni sasa ndipo wizara hiyo imeagizwa ianze ‘kufikiria’.
Mheshimiwa Spika; Kambi Rasmi ya Upinzani inayoongozwa na CHADEMA inaona kauli hizo za Serikali inayoongozwa na CCM ni za kutowajali wazee na za kuwepwa kuwajibika kutimiza ahadi kwamba kuwa tathmini na tafiti zimefanywa mpaka na asasi za kiraia na Serikali kupewa nakala. Aidha, kufuatia tafiti hizo Wizara iliahidi bungeni kwamba wameanza kuandaa mfumo wa kuorodhesha wazee ikiwa ni sehemu ya kuanza kuandaa mchakato wa malipo ya pensheni hizo.
Mheshimiwa Spika; Kambi Rasmi ya Upinzani inayoongozwa na CHADEMA inaitaka Serikali inayoongozwa na CCM kuanza kutoa kauli ya kuanza kulipa pensheni hiyo kwa Wazee mwaka huu 2013 na kuingiza katika bajeti ya mwaka wa fedha 2013/2014 kwa kuzingatia maoni na mapendekezo tuliyotatoa mwaka 2011 na 2012.
Mheshimiwa Spika; Kambi Rasmi ya Upinzani inayoongozwa na CHADEMA inaitahadharisha Serikali inayoongozwa na CCM kwamba ahadi hii isipotekelezwa, tutawakumbusha wazee wote juu ya ahadi alizotoa Waziri Mkuu Mizengo Pinda katika kilele cha siku ya Wazee duniani tarehe 1 Oktoba 2010   alipotumia vibaya nafasi ya kiserikali kutafuta kura za wazee kwa niaba ya CCM ili wazee wafanye maamuzi sahihi ya kukikataa chama hicho. Kambi Rasmi ya Upinzani inayoongozwa na CHADEMA inawakumbusha wazee wote nchini kwamba miaka takribani kumi imepita toka sera ya wazee itungwe mwaka 2003 hata hivyo utekelezaji wake chini ya Serikali inayoongozwa na CCM umekuwa ni wa kusuasua.
8.0 SHERIA ZA KAZI NA HAKI ZA WAFANYAKAZI
Mheshimiwa Spika, tumeendelea kushuhudia kuwepo na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu katika maeneo mengi ya kazi. Tatizo hili limechangiwa kwa kiasi kikubwa na wafanyakazi kutosimamia au kutojua haki zao za msingi kama wafanyakazi na hivyo kusababisha waajiri kutumia fursa hiyo ya wafanyakazi kutozijua sheria, kuvunja sheria na haki nyinginezo za kibinadamu.
Mheshimiwa Spika, Ni muhimu kwa mfanyakazi wa sekta yoyote ile kujua haki zake za msingi kama mfanyakazi na mwajiri kuziheshimu haki za kila mfanyakazi kama zilivyoainishwa katika sheria ya kazi namba 6 ya mwaka 2004 na Sheria za Taasisi za kazi Na.7 ya mwaka 2004. Sote tunatambua kuwa mfanyakazi ni mtu ambaye ameingia mkataba na mtu, taasisi au serikali.Kimantiki, mkataba, kulingana na Sheria ya Ajira Na. 6 ya mwaka 2004 kifungu cha 14 ambayo imetoa aina tatu za mikataba ambayo ni mkataba usio na muda maalum kwa ajili ya watalaam.Mkataba wenye muda maalum kwa ajili ya wafanyakazi wasio kwenye taaluma ya utawala na mikataba kwa ajili ya shughuli maalum kwa muda muafaka na kifungu cha 15 cha Sheria ya Ajira imefafanua kwamba, mikataba yote lazima iwekwe katika maandishi.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo kuna pengo kubwa la sheria katika kulinda haki za wafanyakazi pindi kunapotokea uhamisho wa shughuli yaani(Transfer of Undertakings) kwa upande wa muajiri hususani kwenye sekta binafsi ambapo kumekuwa na migogoro mingi baina ya pande mbili hizi  inayotokana na mapungufu sheria hii.
Mheshimiwa Spika, aidha wakati nikiwasilisha hotuba ya kambi ya upinzani ya wizara hii kwa mwaka 2012/2013 kambi rasmi ya upinzani iliishauri serikali kuleta muswada wa sheria bungeni utakaosimamia maslahi ya wafanyakazi katika suala hili, jambo ambalo linaonekana ni kitendawili mpaka sasa kwa serikali inayojiita siikivu masikioni pa watanzania.
9.0 HAKI NA WAJIBU WA MFANYAKAZI
Mheshimiwa Spika,  mwajiriwa ana haki ya kupata likizo ya siku 28- ambapo kifungu cha 31 kinamtaka mwajiri kutoa likizo ya siku 28 mfululizo kwa kila mwaka wa ajira.Siku 28 hizo zinajumuisha sikukuu iwapo zitaangukia ndani ya siku hizo, na siku za mwisho wa juma. Mwajiri  anaweza kupunguza siku za likizo iwapo mwajiriwa aliomba mwenyewe likizo fupi za muda na ambazo alipokea malipo.
 Mheshimiwa Spika, Ikumbukwe kuwa katika Sheria Ajira, likizo ni suala la lazima kwa kila mfanyakazi na tabia ya kuzuiana likizo kati ya mwajiri na mwajiriwa hairuhusiwi kwani sheria inamlazimisha mwajiri kumlipa mwajiriwa au mfanyakazi fedha ya likizo, ambayo ni nauli ya mfanyakazi, mke wake na watoto wasiozidi wanne na wategemezi wawili,  Katika sheria hiyo ya kazi kuna likizo ya uzazi, kifungu 33, ambapo mfanyakazi atakayekuwa mjamzito anapaswa kutoa taarifa ya maandishi ya miezi mitatu kabla ya kuanza likizo yake ya uzazi na taarifa hiyo ni lazima iambatanishwe na cheti cha daktari. Mjamzito anaweza kuanza likizo yake wakati wowote, ilimradi tu yawe yamebaki majuma manne kabla ya kujifungua .
10.0 MALIPO BAADA YA KUACHISHWA KAZI
Mheshimiwa Spika, mara baada ya kuachishwa kazi, mfanyakazi anatakiwa kulipwa mafao yake yote yanayotokana na ajira yake kwa kipindi chote cha ajira. Malipo hayo ni pamoja na mapunjo ya mshahara, kiinua mgongo na nauli ya kumsafirisha hadi kituo cha karibu na nyumbani kwake. Hata hivyo kumekuwepo na usumbufu mkubwa kwa wafanyakazi wa sekta binafsi na serikali mara baada ya  kustaafu  katika kufuatilia na hata kulipwa stahili hizo jambo ambalo ni ukiukwaji wa sheria ambazo zipo kwa ajili ya kulinda na kuhifadhi haki za wafanyakazi hao
11.0 VYAMA VYA WAFANYAKAZI NCHINI
Mheshimiwa Spika, uhuru wa vyama vya wafanyakazi nchini unatambuliwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uangalizi wa sheria za kazi na Mahusiano ya kazi ya mwaka 2004. Uhuru huu una umuhimu sana katika maeneo ya kazi na historia yake ipo tangu Mapinduzi ya viwanda nchini Uingereza karne ya 19, katika bara la Ulaya na Marekani. Uhuru wa vyama vya wafanyakazi ni msingi muhimu wa haki za binadamu kwa kutoa haki za kila mmoja, kuunda na kujiunga na vyama vya wafanyakazi katika eneo lake la kazi, haki ya kugoma  na kuandamana na maridhiano /matakwa ya kitaifa na kimataifa.
Mheshimiwa Spika, Hata hivyo hali hii ni tofauti kwani vyama hivi vimeendelea kupigia kelele madai na maslahi mbalimbali kupitia vyama vyao lakini Serikali imeendelea kuwa kimya na kukimbilia mahakamani kunyamazisha madai/malalamiko yao, jambo ambalo si suluhisho la masuala hayo bali ni sawa na kujifunika shuka katikati ya mvua kubwa ya mawe huku ukidhani utaikwepa mvua hiyo.
Mheshimiwa Spika, Kambi rasmi ya upinzani tunaitaka na kuishauri serikali kushughulikia kwa dhati masuala yote ya wafanyakazi ikiwa ni malimbikizo ya mishahara, kuboresha mazingira mahali pa kazi na bima za afya kwa wafanyakazi.
12.0 TAKWIMU ZA RASILIMALI WATU NCHINI
Mheshimiwa Spika, katika mkutano wa mwaka wa 47 wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), uliofanyika juni 2012 jijini Arusha,[2] Waziri wa kazi na ajira alisema tatizo la ajira kwa vijana limepungua kutoka asilimia 12.9 mwaka 2000/2001 hadi asilimia 11.7 mwaka 2006. Waziri Kabaka alisema kitendo cha wanasiasa kuendelea kusema tatizo la ajira kwa vijana ni bomu linalosubiri kulipuka, siyo kweli kwani utafiti uliofanywa na wizara yake kwa kushirikiana na Taasisi ya Takwimu ya Taifa (NBS), unaonyesha kuwa tatizo hilo limepungua kwa asilimia 1.2. Waziri aliendelea kueleza kuwa, utafiti uliofanywa na NBS mwaka 2006, kwa kushirikiana na wizara hiyo umebainisha kuwa nguvu kazi ya Tanzania ni milioni 20.6 kati ya watu milioni 37.5, kwa wakati huo.
Mheshimiwa Spika, Ni wazi hali ya uchumi duniani kwa sasa si nzuri hasa kwa nchi zinazoendelea, na changamoto kubwa ni hali ya uchumi pamoja na kubadilika kwa vigezo na masharti katika soko la ajira. Majibu ya serikali kuwa tatizo la ajira kwa vijana limepungua, kwa kuangalia takwimu za mwaka 2006 halitoi taswira halisi ya tatizo hili, hivyo kutoa majibu kwa makadirio ya takwimu kuwa tatizo la ajira limepungua si sahihi. Katika hotuba ya wizara ya kazi na ajira kwa mwaka wa fedha wa 2012/2013 waziri wa kazi na ajira alikiri kuwa tatizo la takwimu za ajira ni changamoto kwa kuwa linaleta picha hasi na aliahidi kuwa wizara yake  kwa kushirikiana na Shirika la Kazi Duniani (ILO) imempata mshauri mwelekezi anaye andaa mfumo wa taarifa za soko la ajira utakaokamilika katika mwaka 2012/2013.[3] na kwa kuwa wakati akijibu swali la Mheshimiwa Naomi Kaihula, tarehe 13 aprili 2011,mheshimiwa naibu waziri wa kazi na ajira alikiri kuwa ni vigumu kupata taarifa za uwiano wa vijana wanaomaliza shule na vyuo na wanaopata ajira kutokana na kukosekana mfumo wa utuatiliaji (Trace Study) kamilifu, ambao ungetuwezesha kufahamu ni vijana wangapi kati ya waliomaliza shule au vyuo wameweza kuajiriwa. Kutokana na upungufu huo, naibu waziri aliahidi kuwa wizara inaandaa mfumo wa upatikanaji wa taarifa za soko la ajira,ambao ungeanza kufanya kazi mwishoni mwa mwaka 2011 na kusaidia kupatikana kwa taarifa hizo.[4]
13.0 WAKALA WA USALAMA NA AFYA MAHALI PA KAZI (OSHA)
Mheshimiwa Spika,OSHA ilianzishwa kwa kutumia Sheria ya  Executive Agencies Act, No 30 ya mwaka 1997. Na wajibu wa OSHA ni kufanya kaguzi na kufuatilia uzingatiaji wa masuala ya usalama na afya na kuhakikisha kuwa waajiri wanazingatia sheria na kanuni za usalama mahali pa kazi hasa Sheria ya Afya na Usalama katika Maeneo ya Kazi (OHS)Na. 5 ya mwaka 2003. Mpaka kufikia Mei 2012, jumla ya kesi 16[5] zilikua mahakamani. Tunaitaka wizara itupe mrejesho wa kesi hizo dhidi ya waajiri waliokiuka sheria na kanuni za  usalama mahali pa kazi.
Kambi rasmi ya upinzani inaitaka Serikali kupitia wizara kuiwezesha OSHA kwa kuipatia rasilimali za kutosha ili iweze kufanya kaguzi zake ikiwemo kutekeleza wajibu wake wa uainishaji na usajili, ukaguzi wa usalama na afya,tathmini za maafa yawezayo kutokea mahali pa kazi na athari zake.
Mheshimiwa Spika, kumekua na matukio mbalimbali ambayo yanatokea nchini ambayo yanasababisha athari si tu kwa raia wengine bali kwa wafanyakazi ambao wanakua ni wahanga wa matukio hayo. Katika kuporomoka kwa jengo la ghorofa 16, jijini Dar Es Salaam ni kielelezo cha kutofanyika pia kaguzi za usalama na afya mahali pa kazi. Lazima Serikali ya CCM ikiri kuwa imeshindwa kuhakikisha kuwa mahali pa kazi ni salama kwa kila mtanzania. Ni fedheha kuwa na wakala wa Serikali mwenye dhamana ya kuhakikisha usalama na afya mahali pa kazi unazingatiwa lakini inashindwa kuwa na vitendea kazi pamoja na rasilimali za kutosha kwa ajili ya kulinda usalama na afya za mahali pa kazi kutokana na ufinyu wa bajeti na rasilimali kazi.
Idadi ya Mahali pa kazi zilizosajiliwa kulinganisha na zisizosajiliwa nchini[6]
Year
Makadirio ya Mahali pa Kazi nchini
Sehemu za Kazi zilizosajiliwa
%ya sehemu za kazi zilizosajiliwa
2009
6,825
1,747
25
2010
11,691
2,069
22
2011
21,068
5,045
24
2012
27,500
6,599
24
Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka wizara, kulipatia Bunge majibu ya maswali yafuatayo kutokana na takwimu zilizopo hapo juu. Je , ni sababu zipi ambazo zimeifanya OSHA ifanye kaguzi za usalama wa afya na mahali pa kazi bila ya kufikia nusu ya sehemu hizo? Na kwa kutumia takwimu ambazo waziri alizitoa katika Bunge hili wakati wa mawasilisho ya bajeti kwa mwaka wa 2012/2013 kwa kutoa taswira kuwa OSHA imefanya asilimia 85.6% ya kazi zilizopangwa kufanyika mahala pa kazi, ni wazi kuwa waziri alikua anaupotosha umma kuwa OSHA imefanikiwa kwenye kusimamia usalama na afya kwa mahali pa kazi, huku ukweli ukiwa kuwa wizara imeshindwa kwa asilimia 76% kusajili mahali pa kazi nchini, hali ambayo inaonesha kuwa si kipaumbele cha Serikali hii ya CCM katika kujali usalama wa watu wake sehemu za kazi.Kambi rasmi inataka kujua ni hatua gani za kisheria ambazo asilimia 75 ya mahali pa kazi ambazo hazijasajiliwa zitachukuliwa kama ambavyo sheria inaelekeza kutoa adhabu? Na je Serikali imeweka mkakati gani wa kuhakikisha kuwa kila mahali pa kazi nchini panasajiliwa? Na kwa kuwa inakadiriwa kuwa kiasi cha shilingi milioni 600 zinahitajika kwa  OSHA ili kuweza kusajili sehemu zote za kazi nchini, je wizara imetenga kiasi gani kwa mwaka huu wa fedha wa 2013/2014?
Mheshimiwa Spika, aidha kambi rasmi ya upinzani inataka kujua pia kama wizara imefanya usimamizi na tathmini ya kaguzi zinazofanywa na OSHA na kama wamefanya tathmini ya shughuli za OSHA, ni vigezo vipi vya ambavyo vimetumia katika kupima na kusimamia utendaji wa OSHA?
14.0 MAPITIO YA UTEKELEZAJI BAJETI 2012/2013 NA MAKADIRIO YA MWAKA 2013/2014
Mheshimiwa Spika, katika fungu 1001 utawala na rasilimali watu katika mwaka wa fedha 2012/2013 zilitengwa jumla ya shilingi 2,780,306,000, aidha kwa mujibu wa randama ya wizara ni kuwa jumla ya shilingi  705,400,000 zilikuwa ni kwa ajili ya kulipia pango la ofisi ya wizara ,maji,umeme na simu na hii ni kwa mujibu wa randama ya wizara shughuli namba D03S01.
Kambi rasmi ya upinzani, inaona kuwa fedha hizi ni nyingi sana kutengwa kila mwaka kwa ajili ya kulipia pango la ofisi ya wizara na ikizingatiwa kuwa ni wizara ambayo inasimamia haki za wafanyakazi ambao kila leo wanalia kutokana na kiwango kidogo cha mishahara , tunataka kujua wizara ina mpango gani wa kujenga ofisi zake ili iachane na mpango wa kulipia mamilioni ya walipa kodi kila mwaka kama pango na ofisi hizo zijengwe Dodoma kama ambavyo serikali mara zote imekuwa ikisisitiza kuwa ofisi zake zitajengwa Dodoma kama sehemu ya maandalizi ya kuhamia Dodoma.
Mheshimiwa Spika, katika fungu hilo hilo la 1001, namba ya mradi D03S08 randama ya wizara inaonyesha kuwa jumla ya shilingi 8,000,000 zilitengwa kwa mwaka wa fedha 2012/2013 kwa ajili ya gharama za safari za waziri na Naibu waziri kwenda Majimboni na hadi mwezi Mei 2013 jumla ya shilingi 5,600,000 zilikuwa zimetumika kwa ajili ya safari tatu za Majimboni kwa Mhe.Waziri na Mhe.Naibu Waziri .
Aidha , kwa mwaka huu wa fedha wizara imeomba kutengewa kiasi cha shilingi 16,710,000 (randama uk 21) kwa ajili ya kuwezesha safari nne za majimboni kwa Mhe.Waziri na Naibu Waziri ,maana yake ni kuwa kila safari moja inatumia wastani wa shilingi milioni nne (4,000,000)hata kwa Naibu waziri ambaye Jimbo lake lipo Ukonga Dar Es Salaam .
Kambi rasmi ya upinzani, inataka kujua kuhusiana na safari ya waziri Jimboni kwani tunajua kuwa huyu ni Mbunge wa Viti maalum na hana jimbo hiyo ziara alifanya kwenye Jimbo gani na fedha za mwaka huu anategemea kwenda kufanya ziara jimbo gani? Aidha , tunataka kujua fedha wanazolipwa kama posho ya mafuta na Bunge kwa ajili ya kufanya ziara majimboni huwa wanazitumia kufanya nini wakati wizarani nako wanajitengea fedha kwa ajili ya kwenda majimboni, ni kwanini wao Mawaziri na Manaibu wawe wanalipwa mara mbilimbili fedha kwa ajili ya kazi moja ? Pia ni mamlaka gani huwa inapanga na kuidhinisha viwango hivyo, au kila wizara inajipangia kutokana na wanavyotaka .
Mheshimiwa Spika, Baada ya kusema hayo kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani, naomba kuwasilisha.
.......................................
Cecilia Daniel Paresso (Mb)
k.n.y Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani-
Wizara ya Kazi na Ajira.
                                                                     29.05.2013

1 comment:

  1. shukrani kwa Mwenyezi Mungu kwa wema wake na wema juu ya maisha yangu nini i wamefanya kama si kwa Bibi Kate Lisa ambaye i daima kuona kama Mungu alimtuma mwanamke ambaye Mungu wamechagua kuwasaidia watu walio katika haja ya fedha kama mimi maskini mjane ambaye alikuwa short waliotajwa, na short wa fedha mwanamke ambao wana watoto wawili na ana majukumu mengi mwanamke ambaye alipoteza mume wake na ina kulipa bili yenye kodi ya nyumba na umeme bili zote mbili na ilikuwa scammed Jumla ya $ 4,000 uSD i kamwe kuamini kwamba bado kuna legit mkopo kampuni online ambao bado wanaamini kwamba watu ni katika tatizo la kifedha na tayari kusaidia baada ya kuwa scammed $ 450,000 uSD i kamwe kuamini kwamba bado kuna legit mkopo kampuni ya mpaka i alimkuta baada ya kuwa alikuwa posted na moja Bibi Luis juu ya jukwaa hiyo yeye alielezea jinsi yeye alipata mkopo wake kutoka Bibi Kate Lisa ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji Bibi Kate Lisa nyumbani mkopo na kisha i mara baada ya hakuna chaguo zaidi kuliko kujaribu bahati yangu kwa wakati wa tatu ili kuepuka kupoteza nyumba yangu (malazi ) ili i kufikiri juu yake i alikuja na hitimisho kwamba i unapaswa kujaribu tena hivyo i kuwasiliana Bibi Kate Lisa kupitia barua pepe wao walihudhuria kwangu katika chini ya 10mins i kutumika kwa ajili ya mkopo jumla ya $ 95,000,00 dola mkopo kupitishwa na ya chini kiwango cha riba na baada ya usindikaji i got mkopo wangu katika akaunti ya benki yangu jana hivyo i unataka haraka kutumia kati ya ushauri yoyote mtafuta mkopo huko nje kuwasiliana na Bibi Kate Lisa email mrskatelisaloanhome1@gmail.com yeye dhahiri kukupa mkopo unahitaji bila matatizo yoyote kwa mara nyingine tena , shukrani kwa Mungu kwa huruma yake juu ya maisha yangu. i itakuwa kuangalia mbele na kusikia ushuhuda wako mwenyewe tu kama yangu.

    Bibi Sarah .

    ReplyDelete

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...