Tuesday, May 14, 2013

HOTUBA YA MSEMAJI MKUU WA KAMBI YA UPINZANI BUNGENI MHESHIMIWA SAID AMOUR ARFI (MB).

 

HOTUBA YA MSEMAJI MKUU WA KAMBI YA UPINZANI MHESHIMIWA SAID AMOUR ARFI (MB), WIZARA YA UJENZI, KUHUSU MAPITIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA 2013/2014 (Inatolewa chini ya Kanuni ya 99(9) toleo la mwaka 2013)


1.0      UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika, jukumu la msingi la Wizara hii ni kusimamia kukamilifu tasnia ya ujenzi kwa ukamilifu wake ili kutoa matokeo bora na kuchochea uchumi wa nchi yetu na kuwaletea maendelo watu wetu na kupunguza umasikini kwa kuwa na miundombinu yenye kukidhi viwango, ubora na Usalama.
2.0      MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA BAJETI 2012/2013
Mheshimiwa Spika, ukusanyaji wa vyanzo vya mapato katika idara na vitengo vya Wizara ya Ujenzi kwa mwaka 2012/13 ulivuka lengo la mwaka hadi kufikia Februari 2013 walikusanya zaidi ya mara mbili ya lengo la makusanyo kwa mwaka. Halikadhalika mfuko wa Barabara ulikusanya takriban asilimia 70 hadi februari 2013 ni dhahiri mfuko wa barabara nao utafikia lengo uliokusudia kwa mwaka 2012/13 na kuvuka lengo, haya si mafanikio haba, hata hivyo hayajakidhi wala kupunguza changamoto za Wizara hii.
Mheshimiwa Spika, matumizi ya kawaida na maendeleo, wizara imeendelea kupokea fedha kwa mtiririko unaoridhisha, matumizi ya kawaida  hadi februari 2013 ilipokea 69% ya fedha za matumizi na 100% kwa miradi ya maendeleo kwa fedha za ndani zilikuwa zimepokelewa.
Mheshimiwa Spika, yapo matukio kadhaa yaliyotokea ambayo Kambi Rasmi ya Upinzani inataka Maelezo ya kina na kutosheleza na hatua zilizochukuliwa ili kuzuia hali hii isijirudie tena na kuleta maafa kwa watanzania. Kambi Rasmi ya Upinzani inatambua majukumu ya Wizara hii pamoja na kuzisimamia taasisi zilizopo chini ya Wizara hii ikiwemo Baraza la Ujenzi (NCC), Bodi ya Usajili wa Wahandisi(ERB), Bodi ya Usajili wa Wabunifu majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQSRB), Pia Bodi ya Usajili wa Makandarasi (CRB) na vyombo hivi kufanya kazi kwa mujibu wa sheria na taratibu za miundo yake.
Mheshimiwa Spika, yamekuwepo matukio ya kujirudia ya kuanguka kwa majengo ya magorofa yaliyokamilika na yanayoendelea kujengwa katika jiji la Dar es Salaam na tukio la hivi karibuni jengo lililokuwa linaendelea kujengwa katikati ya jiji la Dar es Salaam, mtaa wa Indira Ghandi na kupoteza maisha ya Watanzania kadhaa, Kambi Rasmi ya Upinzani inatoa pole kwa wale wote waliopoteza  ndugu na marafiki zao katika tukio hilo Mwenyezi Mungu awapumzishe kwa amani. Aidha,tukio la kuanguka kwa ukuta katika kituo cha Mabasi Ubungo na kuharibu magari na mali za watanzania ambao walifika katika kituo kikuu cha mabasi cha Ubungo kwa kujipatia huduma. Kambi Rasmi ya Upinzani inasikitishwa kwa tukio hilo ambalo lingeweza kuzuilika iwapo mkandarasi angezingatia kanuni za usalama. Tunapenda kuwapa pole watanzania wenzetu waliokumbwa na mkasa huo.
Mheshimiwa Spika, pole na kufarijiana pekee haitoshi bado tunajiuliza kama nchi ni lini viongozi wetu wataheshimu, kuwajibika na kutekeleza majukumu yao na kuwa na ujasiri wa kutafuta mbinu za kutatua matatizo pindi tunapokutana na mambo magumu katika utendaji wetu na si kukimbia  matatizo kwa kujificha  chini ya migongo ya watendaji wengine na kutowajibika na uozo unaotokea katika wizara tunazozisimamia na tukisubiri kusifiwa kwa mazuri yanayofanywa na watendaji haohao na kukwepa lawama kwa mambo ya ovyo.
Mheshimiwa Spika, wakati waziri anawasilisha hotuba yake ya bajeti kwa mwaka wa fedha uliopita alisema kuwa, naomba kunukuu “Bodi itafanya ukaguzi wa kina katika taasisi za elimu ya juu zinazofundisha uhandisi ili kubaini kama vyuo hivyo vina sifa stahiki za kufundisha wahandisi na iwapo wahadhiri wanaofundisha wahandisi wamesajiliwa na Bodi” (Hotuba ya bajeti ya waziri wa ujenzi 2012/2013, uk 162).

Kuendelea bofya Read More


Mheshimiwa Spika, kutokana na nukuu hiyo hapo juu ni dhahiri kuwa wizara na waziri wana hofu na aina ya vyuo vinavyotoa elimu ya uhandisi na pia wana hofu na wahadhiri ambao wanajukumu la kufundisha wahandisi hapa nchini kuwa hawana viwango vinavyotakiwa , Kambi rasmi ya upinzani , tunataka kujua ukaguzi huo ulifanyika katika vyuo gani na hali ikoje na ni hatua gani zilichukuliwa dhidi ya vyuo ambavyo wahandisi na wahadhiri walikutwa hawana sifa sitahiki , kwani tumeendelea kushuhudia maafa yanayotokana na kazi mbalimbali zinazofanywa na wahandisi hapa nchini mwetu.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inahitaji kujua taarifa za uchunguzi ya kuanguka kwa magorofa Dar es Salaam ya mwaka 2006 na hatua zilizochukuliwa baada ya ukaguzi na nyumba ngapi  zilizopaswa kuvunjwa. Kwa maelezo ya Waziri Mkuu mstaafu rejea gazeti la Nipashe la 03 April 2013 ilionekana takriban magorofa 100 katika jiji la Dar es Salaam yalitakiwa kuvunjwa kwa mapungufu na kutokidhi viwango ni magorofa mangapi hadi sasa yamevunjwa?
Mheshimiwa Spika, hivyo basi, Kambi Rasmi ya Upinzani inapendekezaa mambo yafuatayo:-
1.   Hatua stahiki za kinidhamu na kisheria zichukuliwe kwa wahusika wa maafa haya na zionekane zimetendeka ili kujenga  imani kwa watanzania.
2.   Bodi zote nilizozitaja hapo juu ziwajibike ipasavyo kila moja katika eneo lake na kusimamia kikamilifu wajibu wao kwa mujibu wa sheria na taratibu, vinginevyo hatuna sababu ya kuwa na Bodi za kitaalam ambazo haziwezi kusimamia wanachama wao.
3.   Tuangalie upya sheria zetu na ikiwezekana tuwe na mamlaka mahususi ya ukaguzi (Inspection Authority) inayosimamia majengo hususan magorofa yenye kuwa na wataalamu wa fani zote kwa miji na majiji yetu badala ya Halmashauri zetu zinazotoa vibali na kushindwa kusimamia kutokana na ukosefu wa wataalamu ili tuweze kujua ni nani wa kuwajibishwa.
4.   Ukaguzi wa kina na wa kitaaluma ufanywe katika vyuo vyote vinavyotoa elimu ya uhandisi na kuona kama vyuo hivyo vina sifa za kutoa elimu hiyo kwa mujibu wa sheria na kama wahitimu wake wanasifa za kuwa wahandisi.
3.0      MATUMIZI MABAYA YA FEDHA ZA BARABARA
Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya kambi rasmi ya upinzani bungeni kwenye bajeti ya mwaka 2011/2012 tulihoji kuhusiana na fedha zilizokuwa zimetengwa chini ya fungu lililojulikana kama special road construction project” , na tulisema ifuatavyo; Nanukuu hansard ya tarehe 01.08.2011 “Mheshimiwa Spika, Miradi maalum ya ujenzi wa barabara (kasma 4168).kitabu cha Miradi ya Maendeleo (sehemu-A juzuhu iv) katika fungu 98, kasma 4168 utaona kuwa mradi unaitwa “Miradi ya ujenzi wa barabara maalum” (special road construction projects) na fungu hili limetengewa kiasi kikubwa kuliko miradi mingine yoyote ya ujenzi wa barabara katika mwaka huu wa fedha kwani zipo jumla ya sh. 348,075,000,000/= na hizi zote ni fedha za ndani. Kwa hakika hizi ni fedha nyingi sana na hasa ikizingatiwa kuwa kitabu hicho kimeonesha miradi yote ya ujenzi wabarabara ambayo itatekelezwa katika mwaka huu wa fedha, ila hii miradi maalum haijaoneshwa ni miradi ya barabara gani na zitajengwa wapi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kasma hii kwa mwaka wa fedha 2009/2010 na 2010/2011 haikuwa imetengewa kiasi chochote cha fedha na ndio maana imetustua kuona mwaka huu fedha nyingi kiasi hicho zinatengwa kwa miradi isiyojulikana kuwa itajengwa wapi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hata ukiangalia maelezo yaliyotolewa kwenye Kamati ya Bunge ya Miundombinu juu ya mpango na bajeti ya mwaka 2011/2012, kasma 4168 haipo kwenye randama na hakuna maelezo yoyote ambayo yametolewa kuhusiana na fedha hizo ambazo zimetengwa. (Makofi)
Kambi ya Upinzani, tunataka kupata maelezo ya kina ni miradi gani hii ambayo haiwezi kuandikwa na inatengewa fedha nyingi kiasi hicho? Kwani hii italiwezesha Bunge kuweza kupitisha bajeti inayoifahamu na kuisimamia Serikali kwa kuweza kufuatilia utekelezaji wa miradi husika”.
Mheshimiwa Spika, wakati wa mjadala kuhusiana na hotuba ya wizara ya uchukuzi 2011/2012  ilipowasilishwa , Mhe.Mbunge wa Ukerewe Salvatory Machemli alihoji fedha hizi na kusema , naomba kunukuu Hansard ya tarehe 03.08.2011 “Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaja mwanzoni kwamba reli inakufa wakati watu wanaiangalia na Serikali haisemi kitu chochote kazi yao kuomba Miongozo tu hapa, pesa zipo nyingi. Wakati mimi nawasilisha hotuba yangu kwa Wizara ya Ujenzi, nilihoji kiasi cha pesa shilingi bilioni 348 ambazo hazikuonyeshwa zinafanya kazi gani kwenye Wizara ile. Mheshimiwa Magufuli jana wakati anafanya majumuisho hakutaja, amemeza tu japokuwa aliona ni chungu lakini akameza kama chloroquine, nataka sasa hizi shilingi bilioni 348 ambazo zimeonyeshwa kwenye vote 4168 ambazo matumizi yake hazikuonyeshwa basi wapelekewe reli ili tuimarishe reli, tuweze kuokoa barabara zetu kuliko kuziacha tu, jamaa wanatia mfukoni, wanachukua wanaweka waa, kama ilivyo kawaida yenu Chama cha Mapinduzi, mnakwenda kujenga masinagogi Ulaya. (Makofi)”
Mheshimiwa Spika, katika mjadala huo aliyekuwa naibu waziri wa Ujenzi Mhe.Dr.Harison Mwakyembe alijibu kuhusiana na hoja hiyo na kusema , nanukuu hansard ya tarehe 03.08.2011NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ili Mheshimiwa Mbunge asiendelee kupotosha na kujenga mahekalu hewani, nilitaka kumueleza kwamba hizo pesa zilizopitishwa hapa jana ni za Mfuko Maalum ambao unaisaidia Serikali pale ambapo mfadhili wa nje kwa mfano, anaamua kufadhili ujenzi wa barabara fulani na anasema Serikali ichangie ten bilioni, utaitoa wapi kama wewe huna Mfuko Maalum? Serikali ikaona logic ya kuweka Mfuko Maalum ili isitulazimu tena kuitisha Bunge kupitisha pesa hizo, sasa zianze kuleta maneno, kutufanya wote ni wahuni kama yeye na hii siyo vizuri kusema kwamba tutapeleka hizo pesa wapi? Ahsante. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mnamo tarehe 04.08.2011 wakati wa kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Mhe.waziri Mkuu alitoa kauli ya serikali kuhusiana na fedha kuongezwa wizara ya uchukuzi na alisema, nanukuu hansard ya tarehe husika…..’Kwa hiyo, baada ya Kamati ya Miundombinu kupitia Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kuishauri Serikali kuongeza bajeti hiyo kwa shilingi bilioni 95, jambo ambalo tuliliridhia na kulikubali, lakini hatukuweza kufikia kiwango hicho kama ilivyokuwa imeombwa. Kikao cha jana kimewezesha Serikali kufanikiwa kupata fedha hizo ambazo zitatumika kwenye maeneo matatu yafuatayo: Reli ya Kati, Kampuni ya Ndege Tanzania na Usafiri wa Majini yaani Meli katika Maziwa ya Victoria, Tanganyika na Nyasa. Kiasi hicho cha shilingi bilioni 95 ni kiasi ambacho Wizara ilikuwa imeji-commit au imejiahidi mbele ya Kamati kwamba, zikipatikana zitawezesha huduma za msingi katika maeneo hayo matatu kuweza kuendelea bila matatizo makubwa. (Makofi)’
Mheshimiwa Spika, wakati Bunge likiwa limekaa kama kamati ya matumizi wakati wa kupitisha mafungu ya wizara ya uchukuzi Mhe. Tundu lissu aliomba ufafanuzi kama ifuatavyo, nanukuu hansard   “ …..Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nifafanuliwe, kama Bajeti ya Wizara ya Ujenzi ilishapitishwa mafungu yote yalishapitishwa, hii bilioni 95 iliyochotwa kutoka fungu la miradi maalum ya barabara na kuletwa kwenye miradi ya maendeleo ya Wizara ya Uchukuzi ambayo ni Vote tofauti kabisa zimechotwa kwa idhini ya Kanuni ipi, mimi naomba nipewe angalau msingi wa Kikanuni au wa kisheria wa kuchota fedha ambazo tayari zimeshatengwa na Bunge hili bila kupata authorization ya Bunge hili. Ahsante sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, majibu yafuatayo yalitolewa,kwa mujibu wa Hansard  “ WAZIRI WA NCHI OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, URATIBU NA BUNGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu alichokisema Mheshimiwa Tundu Lissu kipo ukurasa 276, Kifungu kidogo cha 4168. Hizi ni fedha ambazo zimewekwa katika Kifungu hiki katika Bajeti hii ya ujenzi lakini ni mfuko maalum, hela hizi hazijawa committed kama unavyoziona. Ukiangalia miradi yote iliyomo katika kfungu hiki ina barabara tayari. Fedha hizi ziliwekwa maalum kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya miundombinu hasa katika maeneo ambayo ipo miradi kadhaa ambayo tuna uzoefu, imekuwa inachangiwa inatolewa na wafadhili, lakini hii tulifikiri sehemu nyingine miradi hii imekwama kwa sababu sisi tulikuwa hatujajitayarisha kuweka counterpart fund. Kwa hiyo, hizi fedha zimewekwa hapa kwa ajili hiyo, miradi yote ambayo Serikali ya Tanzania itafanya kutoka kwenye fedha za wafadhili hizi ni fedha ambazo zimewekwa, ni fungu ambalo haliko committed. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hizi fedha zimechukuliwa hapa zimepelekwa ujenzi kwa maana ya kwamba ni fedha ambazo ziliwekwa kwa ajili ya mfuko wa miundombinu. Zimekuwa voted lakini Mheshimiwa Tundu Lissu atakuja kupata ukweli wa mambo haya yote wakati wa Appropriation Bill. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya fedha hizi kupunguzwa kiasi cha shilingi bilioni 95 na kupelekwa wizara ya uchukuzi zilibakia kiasi cha shilingi bilioni 252.975 katika kifungu hiki, leo tumelazimika kulikumbusha Bunge kuhusiana na suala hili kwani kwa mujibu wa ripoti ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali ya mwaka husika wa fedha kuhusiana na kifungu hiki alisema, naomba kunukuu “malipo ya madeni ya mwaka wa nyuma yaliyolipwa kwa fedha za 2011/2012 kwa kutumia jina la mradi usiohalisi shs.252,975,000,000. Miradi katika wizara ilipewa namba 4168 kwa ajili ya kupitisha malipo ya madeni ya miaka ya nyuma kwa miradi inayotekelezwa na TANROADS. Namba hii sio halisi” (chanzo: taarifa ya CAG uk.160,fungu 98)
Mheshimiwa Spika, fedha hizi “zilizopotea”au “kulipwa kifungu hewa” ni sawa na fedha zote zilizotengwa kwa ajili ya barabara zifuatazo kwa mwaka huu wa fedha 2013/2014;
i.             Barabara ya Usagara-Geita-Kyamyorwa (KM 422)
ii.           Barabara ya Kigoma-Kidahwe-Uvinza-Kaliua-Tabora (KM 443)
iii.          Barabara ya Nangurukuru-Mbwemkulu (KM 95)
iv.          Barabara ya Sumbawanga-Matai-Kasanga Port (KM 112)
v.            Barabara ya Manyoni-Itigi-Tabora (KM264)
vi.          Barabara ya Tabora-Ipole-Konga-Mpanda (KM 359)
vii.        Barabara ya Kidatu-Ifakara-Lupilo-Malinyi-Londo-Lumecha/Songea(KM- 396)
viii.       Kuondoa msongamano barabara za Dar (KM- 102.15)
Aidha, ni sawa na kusema kuwa barabara ya lami yenye urefu wa kilomita 316.218 imepotea kwa kutumia mahesabu ya wizara ya ujenzi kuwa kilomita moja ya lami inajengwa kwa kiasi cha shilingi milioni mia nane (800,000,000), hii ni sawa na kusema kuwa barabara ya kutoka Manyoni-Itigi-Tabora (KM 264) Changanya na barabara ya kutoka Chunya –Makongorosi (KM 43) na Barabara ya Tangi Bovu –Goba (KM 9), zimepotea kutokana na ufisadi huu.
Kambi rasmi ya upinzani, inataka kupata majibu yafuatayo kuhusiana na suala hili;
i.             Fedha hizi zilizokuwa zimetengwa zilitumika kwa ajili ya kufanyia shughuli gani? Kwani majibu yaliyotolewa na wizara na serikali Bungeni sio yaliyotolewa kwa mdhibiti na Mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali
ii.           Ni madeni gani yalilipwa kama kweli yalikuwepo?au wajanja wachache walijinufaisha ? na wahusika wamechukuliwa hatua gani mpaka sasa.
iii.          Nini kauli ya serikali kuhusiana na Ufisadi huu, mbele ya Bunge na watanzania kwa ujumla .
iv.          Je, Tunaweza kuendelea kuamini kauli za viongozi wa serikali hii ndani ya Bunge kama hii ndio hali halisi ?
v.            Nini kauli ya serikali kuhusiana na Ufisadi huu.
4.0      MFUKO WA BARABARA
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inatoa pongezi kwa Mwenyekiti, Bodi na Watendaji wa Mfuko wa Barabara kwa kazi nzuri wanayoifanya kwa uwazi na uwajibikaji. Kambi Rasmi ya Upinzani inapendekeza kutafuta njia bora ya kuongeza mapato kwa mfuko huu ili uongeze kasi ya kusaidia Ujenzi wa Barabara zetu na matengenezo. Aidha, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kukusanya fedha za tozo  kutoka makampuni ya uchimbaji wa madini ambayo ndio waaribifu wakubwa wa barabara zetu kwa kusafirisha mizigo mizito na magari makubwa na kufutiwa msamaha wa tozo hilo kama watumiaji wakubwa wa mafuta, huku wafanyakazi na wafanyabiashara wanatozwa tozo hilo kila wanaponunua mafuta, kwa kutoa msamaha kwa makampuni haya yanaukosesha mfuko wa Barabara kiasi kikubwa cha fedha.
4.1      Matumizi mabaya ya fedha za Mfuko wa barabara.
Mheshimiwa Spika, pamoja na mfuko wa barabara kujitahidi kukusanya mapato kwa wingi, ila pia kasi ya matumizi ya fedha hizo kwa ajili ya masuala ambayo sio ya kujenga barabara moja kwa moja imeongezeka sana, kwa mfano kwa mwaka huu wa fedha kwa mujibu wa randama  kiasi cha shilingi bilioni 9.126 zilizotengwa (tazama kiambatanisho A ni Jedwali na 4) ni kwa ajili ya miradi inayotekelezwa kwa kutumia fedha za mfuko wa barabara (5.5.2.1 Barabara Kuu), kati ya fedha hizo Kiasi cha shilingi bilioni 2.460 kitatumika kwa ajili ya matumizi ambayo siyo ya kujenga barabara moja kwa moja kama ifuatavyo;
i.             kifungu cha 2326,training and Technical assistance TANROADS Shilingi milioni 300.00 , hizi ni kwa ajili ya kutoa mafunzo ya kitaalam kwa wafanyakazi 100 wa TANROADS
ii.            Kifungu 2326, updating of draft design manual 1989 and economic analysis manuals for TANROADS ,shilingi milioni 300.00
iii.          Kifungu 2326,vifaa vya maabara,ufuatiliaji na usimamizi wa kazi za ujenzi wa barabara shilingi milioni 500.00
iv.          Kifungu 2326, kuandaa mpango mkakati wa TANROADS kwa kipindi cha miaka mitano shilingi milioni 100.00
v.           Kifungu 2326,ufuatiliaji na usimamizi wa kazi za ujenzi wa Barabara TANROADS shilingi milioni 400.00
vi.          Kifungu 2326, ufuatiliaji na usimamizi wa miradi (monitoring and other related activities ) shilingi milioni 860.00
Mheshimiwa Spika, Aidha, kwa upande wa barabara za mikoa Fedha za mfuko wa barabara ambazo zitatumika kwenye mambo ambayo sio kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa moja kwa moja wa barabara ni kiasi cha zaidi shilingi bilioni 2.465 ,tazama kiambatanisho B uk. 26 &27
Kambi rasmi ya Upinzani, inataka kujua mambo yafuatayo;
i.             Kwanini fedha za mfuko wa barabara hazielekezwi zote kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa barabara ?
ii.            Mbona fedha kwa ajili ya kufuatilia na kusimamia miradi ni nyingi sana wakati kwenye mikataba ya ujenzi fedha za usimamizi wa mradi huwa zipo?
iii.          Je? Ni kwanini fedha kwa ajili ya mafunzo, uandaaji wa nyaraka mbalimbali za wizara zisitokane na fungu la serikali kuu na fedha za mfuko wa barabara zikawa ni kwa ajili ya kuwekezwa zote kwenye sekta husika , yaani ujenzi na ukarabati wa barabara na si matumizi mengine.
5.0      MSONGAMANO JIJI LA DAR ES SALAAM
Mheshimiwa Spika, kama Taifa tunapoteza wastani wa masaa 4 kila siku za kufanya kazi ukiwa barabarani sawa na siku 112 za kazi kwa mwaka, hiki si kiasi kidogo katika nchi maskini inayohitaji maendeleo kwa haraka kuzipoteza barabarani badala ya kutumika katika uzalishaji, na wafanyakazi kulipwa mshahara kamili wa masaa 8 ya kazi wakati amefanya kazi kwa masaa 4 tu, Taifa linapoteza kiasi kikubwa katika ujira, watumiaji wa barabara wanatoa fedha zaidi kufika mahali anapokwenda kwa kuchoma mafuta akiwa amesimama barabarani muda mrefu sana na hasara hii haipimiki.
Mheshimiwa Spika, hivyo basi, Kambi Rasmi ya Upinzani inapendekeza yafuatayo:-
1.   Kasi ya Ujenzi wa Mradi wa DART(Mabasi yaendayo kasi Dar) iongezwe ili mradi huu ukamilike kwa haraka kupunguza  tatizo la msongamano Dar.
2.   Miradi ya barabara za viungo (Ring Roads) ikamilishwe na kutazama barabara mpya zitakazosaidia kupunguza msongamano.
3.   Kutafuta fedha maalum(Special fund) hata kwa kukopa kwa ajili ya barabara za Dar es Salaam na kuzijenga upya na kujenga barabara za juu (Fly overs) badala ya kusubiri wahisani hata kujenga KM 3 toka UDA depot/Kamata junction tunasubiri fadhila na hisani, hii ni aibu kwa Taifa letu.
4.   Upanuzi wa barabara unaooendelea sasa uzingatie mahitaji ya baadae na si sasa. Kila panapostahili tujenge njia zaidi ya mbili kila upande, tuachane na mazoea ya njia 2 twende njia 3 au 4 kila upande wa barabara na Jambo hili lianze sasa.
Mheshimiwa Spika, kwa fedha zinazotengwa katika bajeti za kila mwaka ya Wizara hatuwezi kumaliza tatizo la barabara za Dar es Salaam, Serikali ichukue maamuzi magumu ya kuwa na fedha za kutosha (special fund) kwa tatizo la Dar es Salaam mji unakua kwa kasi kubwa.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali na Wizara hivi sasa kuwasilisha Bungeni mipango ya muda mfupi/Kati/ mrefu wa kukabiliana na changamoto za kukua kwa miji ya Arusha, Mwanza na Mbeya na tatizo la msongamano ambao umeanza kujitokeza katika miji hiyo, ili tuweze kujiandaa mapema badala ya kusubiri mpaka hali iwe mbaya ndipo tuanze kuchukua hatua za dharura.
6.0      DARAJA LA KIGAMBONI
Mheshimiwa Spika, katika ujenzi wa daraja  hili la Kigamboni Kambi Rasmi ya Upinzani inaipongeza NSSF na wadau wengine kwa kuona umuhimu wa daraja hili na kuchukua tahadhari ya mahitaji ya baadae kwa kuongeza njia katika kila upande wa Barabara hiyo lakini Wizara inapaswa kujipanga sasa namna ya kukabiliana kuyaondoa magari mengi yatakayokuwa yanatumia barabara hiyo, vinginevyo itakuwa haina tija  kwa maana utakwenda kasi darajani unakuja kukwama uhasibu junction (Mandela/Kilwa Rd) na Uda Depot(Mandela road)
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inataka kupata maelezo, ratiba na maandalizi ya kukabiliana na changamoto hiyo ili mradi huu uweze kuleta tija kwa taifa.
7.0      MIRADI YA UJENZI WA BARABARA
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya Wizara, Wizara ilipokea fedha zote 100% kwa ajili ya miradi ya maendeleo kwa mwaka 2012/13, hata hivyo Kambi Rasmi ya Upinzani inasikitishwa kwamba fedha iliyoombwa haikutumika katika miradi mingi iliyoombewa fedha mwaka 2012/13 na kutokamilika kwa miradi hiyo hususan barabara za Dar es Salaam kama vile barabara ya Kimara-Kilungule,Mbezi-malamba mawili-Kinyerezi, Banana-Tegeta, Kibaoni-Wazo-Goba, Mbezi Morogoro-Tangibovu-Goba na Kimara Baruti.
Mheshimiwa Spika, wananchi wamechoshwa na hotuba za Mawaziri zenye matumaini,ahadi na maneno mengi huku wakijua na kuamini kwamba hawatatimiza wajibu wao na kulidanganya Bunge na kuwapa wananchi matumaini yasiyotekelezeka. Kambi Rasmi ya Upinzani inashauri miradi inayoombewa fedha na kuidhinishwa na Bunge itekelezwe kwa mujibu wa mpango wa bajeti na si vinginevyo.
Mheshimiwa Spika, miradi ya barabara kuu, kadhalika haijengwi kwa kasi inayotakiwa, miradi mingi ambayo ilikuwa ikamilike mwaka 2012, 2013 na mapema 2014 bado haijakamilika hadi sasa. Ujenzi wa barabara nyingi kati ya hizo umefikia chini ya asilimia 50% ya ujenzi, kama Barabara ya Sumbawanga/Kibaoni, Sumbawanga/Kasanga, Tabora/Nzega, Tabora/Ndono, Ndono/Urambo, Kyaka/Bugene/Kasulo. Manyoni/Itigi/Chaya,Tabora/Nyahua, Korogwe/Handeni, Korogwe/ Mkumbara, Mkumbara/Same, Mbeya/Lwanjilo, Lwanjilo/Chunya,Chalinze/ Kitumbi, Mhe Spika, orodha ni ndefu, lakini zipo pia ambazo zimejengwa kwa kiwango cha kati ya 45%-70% kadhalika orodha ni ndefu kwa ujumla miradi yetu yote ya barabara haikamiliki kwa wakati ni pamoja na barabara ya Iringa/ Dodoma/Kondoa/Babati.
Mheshimiwa Spika, hivyo basi, Kambi Rasmi ya Upinzani  na watanzania kwa ujumla wanataka kujua juu ya masuala yafuatayo:
a.   Kwa nini miradi hii haijakamilika kwa mujibu wa mikataba iliyopo, aidha wanataka kujua hasara inayopatikana kutokana na kutokamilika kwa miradi hii kwa wakati.
b.   Gharama halisi ya miradi hii hadi sasa imeongezeka kwa kiasi gani kulinganisha na gharama za awali kutokana na kuchelewa kwa miradi hii ?
c.   Zipo taarifa kuwa baadhi ya miradi iliyokamilika na kutumika bado ina madeni, je? inadaiwa kiasi gani na lini italipwa?
d.   Watanzania wanataka kujua jumla ya riba na deni tunalodaiwa katika miradi ya barabara ni kiasi gani mpaka sasa na kuna mkakati gani wa kulipa deni hilo?
e.   Serikali itoe maelezo ya kina ni sababu zipi zilizopelekea kampuni ya Progressive kupewa mkataba wa kujenga barabara ya Tunduma/Matemanga/ Kilimasera/Namtumbo ambayo iligawanywa lot 3 na zote kupewa kampuni moja, mbaya zaidi  kampuni hiyo haikuwa na sifa ya kujenga barabara, katika nchi za Afrika, nani aliitambua, nani aliileta nchini, nani aliwasaidia kupata kazi na kwanini wameshindwa. Je muda na hasara tunayopata na kuchelewa kwa mradi kwa hatua zilizochukuliwa nani analipa na nani kawajibishwa  kwa uzembe huu.
f.    Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Wizara kutoa ratiba na mpango mkakati wa kufungua kanda ya Kusini na Magharibi kwa barabara ya Masasi hadi Mbamba-bay. Tabora/Mbeya, Tabora/Mpanda, Mpanda/Kogoma na Kigoma/Biharamulo.
g.   Ujenzi wa barabara uzingatie michoro, sheria za ujenzi wa barabara na kuondosha mara moja matuta madogo madogo katika barabara kuu, maarufu kama Rasta zinaleta uharibifu mkubwa  kwenye vyombo vya usafiri na inapokuwa lazima, wajenge Bumps zenye uwiano kwa barabara zote na  kuwepo alama za barabarani. Hakuna barabara kuu (Highway) yeyote duniani iliyo na rasta na  Bumps ila Tanzania, tunaona BUMPS katika barabara za mijini na si  high way.
Mheshimiwa Spika,  Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali miradi yetu yote izingatie mpango wa Taifa wa miaka 5, na uwezo wa kifedha wa nchi. Wataalam watimize wajibu wao na wasiwe  watumwa wa kauli na ilani za kisiasa-Mwalimu alisema, “Kupanga ni kuchagua” –ukishindwa kuchagua huwezi kupanga.
8.0      TANROADS
Mheshimiwa Spika, wakala huu ni muhimu sana katika kusimamia na kuendeleza ujenzi wa Barabara nchini, kwa mujibu wa Taarifa ya ukaguzi wa utendaji ya PPRA kwa 2011/2012 inasema kuwa Tanroads kwenye kipengele cha kusimamia ubora (compliance level and Quality Control) imepewa alama 45 kati ya 100, PPRA imeshindwa kupata taarifa za kumbukumbu kwamba Tanroads ina mpango wowote wa kusimamia ubora wa kazi kwenye mikataba inayotolewa. Aidha kwenye kipengele cha mikataba (compliance on contracts Management) imepewa alama 0 kati ya alama 100, kwa maana kwamba PPRA hawakuona ushahidi wowote kwamba Mamlaka imekuwa ikisimamia mikataba kwa bidhaa na huduma zinazotolewa kwa mujibu wa mikataba na wakandarasi
Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kwamba kwa hali hii bado tutaendelea kushuhudia mikataba mibovu, ujuzi chini ya kiwango, hasara kwa taifa na kupungua kwa kasi ya maendeleo ya nchi.
Mheshimiwa Spika, hivyo basi, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Wizara ya Ujenzi kushughulikia mapungufu hayo na kuondoa dosari zilizopo kwa kupata wataalam wenye sifa, uwezo na weledi katika maeneo yenye mapungufu na kutoa fursa za mafunzo kwa wataalam waliopo, aidha uongozi na utawala uimarishwe.
9.0      WAKALA WA BARABARA VIJIJINI
Mheshimiwa Spika, tunatambua barabara vijijini zinasimamiwa na Halmashauri zetu ambazo nyingi hazina uwezo mkubwa wa kifedha na pia hutengewa fedha kidogo na mfuko wa barabara kulingana na kazi kubwa wanayotakiwa kufanya ya kuhakikisha kuwa barabara zinapitika katika kipindi chote cha mwaka mzima, Aidha wana ukosefu mkubwa wa nyenzo na wataalam. Kutokana na umuhimu wa barabara hizi kwa uchumi wa wananchi wetu ambao wanaishi vijijini , kwa mara nyingine tena Kambi Rasmi ya Upinzani inapenda kuishauri Serikali na kupendekeza kuwepo na WAKALA WA BARABARA VIJIJINI (RURAL ROADS AGENCY) kwa ajili ya usimamizi, ufanisi na ujenzi wa barabara bora vijijini.
Mheshimiwa Spika, Kwa kufanya hivyo tutaweza kufungua uchumi wa vijijini kwani kutakuwa na wakala ambaye atakuwa na jukumu la kuhakikisha kuwa barabara zinafanyiwa matengenezo na ukarabati kwa wakati na hivyo kurahisisha uchukuzi wa mazao ya vyakula kutoka maeneo ya uzalishaji na kuweza kuwafikia watumiaji wa mazao hayo yakiwa katika hali ya ubora zaidi na hivyo yataweza kuongezewa thamani kulingana na ubora wake .Aidha, tutaweza kuchochea uzalishaji kwa kiwango kikubwa kwani maeneo mengi ya vijijini mazao huharibika kutokana na kukosekana kwa barabara na hivyo kuwakatisha tamaa wakulima/wazalishaji, pia Taifa litakuwa na uhakika wa barabara/madaraja yatajengwa katika kiwango cha kuridhisha na thamani ya fedha(value for money) kuonekana na kupimika.
10.0  VIVUKO NA MADARAJA
Mheshimiwa Spika, katika eneo hili juhudi zimefanyika kwa kiwango ambacho si cha kuridhisha sana pamoja na changamoto zake, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Wizara kuagiza na kusimamia kwa uangalizi mahususi kuhakikisha madaraja yote yanayojengwa yanakamilika kwa wakati. Ubora na usalama kwa vivuko vyetu vyote nchini uimarishwe, matengenezo yafanyike kwa wakati, vifaa vya usalama viwepo vya kutosha, pia ukaguzi wa mara kwa mara uimarishwe na uthibiti wa idadi ya abiria na mizigo uzingatiwe.
Mheshimiwa Spika, kwa umuhimu wa mahitaji ya kipekee na haraka, Mv Ilagala  ni kidog na chakavu kimekuwa kikiharibika mara kwa mara ni lini kivuko cha uhakika kitapelekwa licha ya kuwepo kwa ahadi nyingi, au kujenga daraja katika mto Malagarasi kama mto Kilombero ili kuondoa adha hiyo?
Mheshimiwa Spika, katika hotuba yetu ya Kambi Rasmi ya Upinzani kwa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa tulishauri kwamba,Kikosi cha Wanamaji (Navy) kinatumika chini ya Kiwango. Licha ya kikosi hiki kuwa na wahandisi wa usafiri majini waliobobea, Serikali hii ya CCM imekuwa ikitoa zabuni za kutengeneza vivuko kwa wakandarasi wengine kwa gharama kubwa wakati wanajeshi wenye taaluma hiyo wapo.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kutoa zabuni za kutengeza vivuko kwa kikosi cha wanamaji kwa kuwa wana taaluma hiyo, na pia kwa kufanya hivyo wanapata nafasi ya kufanyia mazoezi taaluma zao”.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa jukumu la vivuko, madaraja na barabara liko chini ya Wizara hii ya Ujenzi, hivyo Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Wizara kulifanyia kazi pendekezo hilo ili kuangalia ni kwa jinsi gani kamandi hii ya navy itakavyoweza kutekeleza jukumu hilo la utengenezaji na ukarabati wa vivuko.
11.0  TAMESA
Mheshimiwa Spika, kitengo hiki ni muhimu sana katika kuthibiti matumizi bora ya fedha za umma katika matengenezo ya magari ya Serikali kuu na Serikali za mitaa. Sehemu kubwa ya matumizi ya Serikali yanagusa usafirishaji na upo mwanya wa ubadhirifu, wizi na matumizi mabaya katika gharama za uendeshaji wa sekta ya usafiri katika Serikali na kulipa gharama kubwa za matengenezo katika karakana na makampuni binafsi.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inapendekeza kwamba:
i.        Serikali ifanye maamuzi bila ya kuchelewa kukiimarisha kitengo hiki kwa raslimali fedha na watu (wataalamu), nyenzo na majengo ya karakana  ili magari yote yatengenezwe kupitia wakala huu kama ilivyokuwa zamani na kupiga marufuku magari ya Serikali kufanyiwa matengenezo katika karakana binafsi.
ii.      Wakati Serikali inajipanga kutekeleza hilo, kama imeweza kusimamia kuagiza mafuta  nchini kwa utaratibu wa Bulk Procurement, Serikali iiwezeshe TAMESA kufanya “Bulk Procurement” ya Matairi ya magari kwa ajili ya Serikali. Jambo hili si gumu hata kidogo ili kuwepo na bei inayofanana, na ubora wa matairi kwa magari ya Serikali/Halmashauri badala ya kila idara, Wizara, Taasisi kununua kwa bei wanayoikuta sokoni na yenye kupishana kwa kiwango kikubwa na ubora.
12.0  WAKALA WA MAJENGO(TBA)
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha uliopita 2012/2013 waziri wakati anawasilisha hotuba yake ya bajeti alisema kuwa wakala wa majengo uko katika mchakato wa ujenzi wa nyumba 10,000 katika mikoa yote kwa ajili ya kuishi watumishi wa umma .Aidha , alisema kuwa katika mwaka huo wa fedha wizara kupitia wakala wa majengo ilikuwa imepanga kujenga nyumba 2,500 katika mikoa yote ya Tanzania Bara na fedha kwa ajili ya kukamilisha mradi huo zilikuwa tayari zimepatikana, kama mkopo kutoka kwenye Mabenki ya ndani ambayo TBA ilikuwa imeomba .
Mheshimiwa Spika, waziri alisema katika hotuba yake ya bajeti kwamba, naomba kunukuu “Aidha katika mwaka wa fedha 2012/2013 wizara kupitia wakala wa majengo Tanzania imepanga kujenga nyumba 2,500 katika mikoa yote ya Tanzania Bara”(ukurasa 159 aya 230), hakika maneno haya yalikuwa faraja kwa watumishi na matumaini kwa watanzania.
Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni, inataka kujua majengo hayo 2,500 ambayo yalikuwa tayari yametengewa fedha kwenye bajeti iliyopita yamejengwa katika mikoa gani na maeneo gani hapa nchini, Je? Nyumba hizo wamepewa watumishi wa kada gani na ni vigezo gani vilitumika katika kugawa  nyumba hizo kwa watumishi hao.
13.0  HITIMISHO
Mheshimiwa Spika, kumekuwepo malalamiko na kutokuridhishwa na hatua zinazochukuliwa na Wizara na Taasisi zake hususan Tanroads kutowalipa wananchi fidia stahiki, za haki na kwa wakati wananchi hawaridhishwi na kauli za viongozi wa Wizara hususan katika suala la kuwalipa wananchi fidia kwa mali zao wakipisha miradi mbalimbali za ujenzi nchini.
Mheshimiwa Spika, miradi ya ujenzi, na hasa barabara za lami ni maendeleo kwa jamii pana na Taifa, kwa mwananchi wa kawaida maendeleo kwetu ni nyumba/shamba/ardhi yake hata kama nyumba ni ya miti, tofali za tope na kuezekwa kwa nyasi kwake ni maendeleo na si barabara ya lami, unapomvunjia/kunyang’anya ardhi yake unamzidishia mtanzania huyo umaskini kwa gharama ya maendeleo ya jamii pana. Kwa sababu yoyote ile, kwa namna yoyote ile haki yake ni lazima narudia ni lazima alipwe, kitendo chochote cha kuvunja au kunyang’anya mali ya mtu yeyote ni dhulma kama inafanywa na mtu au Serikali ni dhulma.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani kamwe haiwezi kukubali, kushangilia au kushiriki katika dhulma hii, tunasema walipeni haki zao hawa watanzania maskini ambao mali mnazoziharibu na kunyang’anya ndio maendeleo na ustawi wa maisha ya familia zao, na kama kweli Serikali ya CCM inavyodai maisha bora kwa kila mtanzania, basi boresheni maisha ya watanzania hawa kwa kuwalipa stahiki zao ili waweze kupata makazi/Ardhi mbadala, waondoleeni watanzania hawa mifadhaiko ya maisha na chuki dhidi ya Serikali.
Mheshimiwa Spika, chakula, nguo, malazi ni haki za msingi kwa kila binadamu, hata kama ni kibanda ndiyo makazi yake, hakuna mtu yeyote mwenye haki ya kumnyang’anya   mwingine haki hizo bila ya kufidia au kumpatia makazi mbadala. Kilio cha fidia, fidia zisizostahiki, fidia za upendeleo na kutokulipwa ndio kilio cha watanzania kila kwenye mradi wa ujenzi hususan Barabara. Orodha ni ndefu ya wananchi wanaolalamika kila palipo na mradi na hata waliokuwa tayari kupisha mradi kwa ahadi ya kulipwa wanaendelea kusumbuliwa na urasimu wa Tanroads, Wizara na Hazina, walipeni wananchi haki zao mapema.
Mheshimiwa Spika, mihimili ya dola kila mmoja ufanye kazi bila kuingiliwa na kuheshimika. Wizara hii na Tanroads haipo juu ya sheria na inatakiwa kuheshimu sheria hata pale panapotolewa tangazo (notice) ya kukusudia kuishtaki Serikali kabla serikali haija wasilisha majibu katika vyombo vya haki. Wakala wa barabara anavunja nyumba za watanzania maskini tena wenye hati miliki ya viwanja zilizotolea na mamlka za Serikali hii kabla shauri kusikilizwa mahakamani, huu ni ukiukwaji mkubwa wa haki za raia, kuheshimiwa utu wake na kusikilizwa. Wizara hii isiwaongezee watanzania umaskini. Wakaazi wa Minsukumilo/Mpanda Hotel ni wahanga wa ubabe huu wa kutoheshimu mamlaka nyingine.
Mheshimiwa Spika, kuwepo kwa sheria ni jambo moja, kusimamia sheria ni jambo lingine.  Uungwana na lugha njema ni zaidi ya hayo, kwa kuwa Wizara ilishindwa kutambua na kuweka mipaka ya maeneo yao toka sheria ilipotungwa mwaka 1926, leo wanamlaumu nani kuvamia maeneo yao, sasa ndio wanakumbuka kwamba wanamaeneo ambayo tayari ni makazi ya wananchi si kisingizio cha kuwapora haki zao, wangeliweka mapema mipaka ya hifadhi ya barabara wananchi wasingelijenga wangeheshimu mipaka hiyo iliyokuwepo vingenevyo wizara inakwepa uzembe wake kwa kuwaadhibu watanzania maskini.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kulipa fidia kwa wote sio watu wa Dar es Salaam walipwe fidia. Watanzania wote wanahaki sawa mbele ya sheria, Kambi Rasmi ya Upinzani hairidhiki na watanzania maskini kutolipwa fidia katika miradi mbalimbali ya barabara nchini, fidia stahiki na kwa wakati.
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani, naomba kuwasilisha.
…………………………………..
Said A. Arfi (Mb)
Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani- Wizara ya Ujenzi
                                                                              13.05.2013

Source:CHADEMA social media.

No comments:

Post a Comment

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...